Waziri Jafo: Tumeendelea Kupata Kupata Mafanikio Makubwa Kupitia Muungano

Aug, 21 2023

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo amesema mafanikio makubwa ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi yameendelea kupatikana kufuatia kupatikana kwa ufumbuzi wa hoja za Muungano katika vikao vya majadiliano vilivyoanza kuanzia mwaka 2006 hadi sasa.

Akizungumza na Wajumbe wa Kamati ya Sheria, Utawala Bora na Idara Maalum za SMZ wa Baraza la Wawakilishiwaliotembelea Ofisi ya Makamu wa Rais Mji wa Serikali, Mtumba Jijini Dodoma, tarehe 21 Agosti, 2023), Waziri Jafo amesema kupatikana kwa mafanikio hayo ni jambo la kujivunia kwa kuzingatia historia ya ufumbuzi wa hoja za Muungano zilizokuwepo awali.

Kwa mujibu wa Waziri Jafo amesema ndani ya kipindi cha miaka miwili ya Uongozi wa Serikali ya Awamu ya Sita na Serikali ya Awamu ya Nane ya Mapinduzi Zanzibar, kumekuwa na kasi ya kubwa ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo imeleta mafanikio makubwa kwa wananchi ambayo imeleta matunda na faida kubwa kwa manufaa ya wananchi wa Tanzania Bara na Zanzibar.

“Nilipofanya mahojiano na ZBC kule Zanzibar nilieleza kwa undani namna miradi ya fedha za UVIKO 19 zilivyoleta mageuzi makubwa katika sekta za elimu, afya na maji kwa kugusa maisha ya wananchi na hii ilitokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali zetu…Sasa tunapata taswira kuwa Muungano wetu umeendelea kuzaa matunda makubwa” amesema Dkt. Jafo.

Aidha Waziri Jafo amebainisha mafanikio mengine yaliyopatikana kwa upande wa Zanzibar ni pamoja na utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa uwanja wa ndege Pemba sambamba na utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa mtandao wa barabara Zanzibar, miradi ambayo inasimamiwa na kutekelezwa na kupitia uwekezaji wa Serikali.

Dkt. Jafo amebainisha kuwa kutokana na kasi kubwa ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa sasa Zanzibar, hadi kufikia mwaka 2024 taswira ya mwonekano wa Zanzibar itakuwa ni tofauti hatua itayovutia na kushawishi wawekezaji wakubwa kuweza kujitokeza kutokana kuimarisha kwa miundombinu ya huduma za kijamii na kiuchumi.

“Hatuna budi kuwashukuru Viongozi wetu Wakuu kwa kuendelea kutusimamia vyema kutokana na maelekezo yao kwetu….Tumeendelea kufanya kazi kwa karibu sana na kamati zetu zinazosimamia Ofisi hii ili kuhakikisha tunashughulikia hoja zote zitakazowasilishwa na wajumbe” amesema Dkt. Jafo.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hamza Hassan Juma alimshukuru Waziri Jafo kwa juhudi kubwa zinazoendelea kufanywa na Ofisi yake katika kuratibu na kusimamia masuala mbalimbali ya Muungano kwa kuweka msisitizo wa kusikiliza na kutatua hoja mbalimbali zinazoibuka na kujitokeza katika mijadala ya majukwaa mbalimbali.

“Nilipoleta mwaliko katika Ofisi yako kuja kukuona nikiwa na wajumbe wa kamati, ulikubali hoja yangu na ulionesha wazi nia yako ya kukutana ana kwa ana na wajumbe pamoja na ratiba yako kuwa na mwingiliano wa majukumu ya ofisi….Nikushukuru kwa fursa hii na pia ni kiashiria cha dhamira tuliyonayo katika kuratibu vyema masuala ya Muungano wetu” amesema Mhe. Juma.

Naye Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Khamis Hamza Khamis amesema Ofisi hiyo imeendelea kutekeleza vyema majukumu yake katika kusimamia na kuratibu wa masuala ya Muungano na Mazingira ambapo mafanikio makubwa yameendelea kupatikana kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali inayogusa maisha ya wananchi.

“Tumeendelea kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati kama mnavyojionea na Muungano wetu pia umeendelea kuimarisha na hii inaonesha juhudi kubwa zinazoendelea kufanywa na Viongozi wetu Wakuu akiwemo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na Rais wa Zanzibar Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi” amesema Mhe. Khamis.

Mwenyekiti wa Kamati ya Sheria, Utawala Bora na Idara Maalum za SMZ wa Baraza la Wawakilishi Mhe. Machano Othman Said aliipongeza Ofisi ya Makamu wa Rais kukubali mwaliko wa kutembelea ofisi hiyo na kusifu juhudi kubwa zinazoendelea kufanywa na Serikali ya SJMT na SMZ katika kutekeleza miradi ya maendeleo ikiwemo upatikanaji wa fedha za miradi ya UVIKO 19 ambayo imeleta manufaa makubwa kwa wananchi wa Zanzibar.

“Leo kila Jimbo Zanzibar lina mradi wa madarasa unatokana na fedha za UVIKO, na pia hakuna jimbo lililokosa mradi wa barabara….Tunawasihi Mawaziri wetu mnaosimamia Wizara hizi muendeleze mashirikiano ili wananchi wetu waendelee kupata manufaa ya kwa kuwa ndio dhamira ya Viongozi wetu wakuu” amesema Mhe. Machano.

Settings