Waziri Jafo aridhishwa mazingira Mradi wa SGR Dodoma

Sep, 02 2021

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Selemani Jafo amefanya ziara ya kukagua uzingatiaji wa hifadhi ya mazingira Mradi wa Reli ya kisasa katika maeneo ya Iyumbu na Mkonze leo Septemba 2, 2021 jijini Dodoma

Akikagua mradi huo unaotekelezwa na Shirika la Reli ya Tanzania (TRC) pamoja na mambo mbalimbali alisema kuwa ameridhishwa na namna mradi huo unavyozingatia matakwa ya hifadhi ya mazingira.

Alisema pamoja na mradi huu kuwa mzuri, nia ya Serikali ni kuhakikisha unasonga mbele na kukamilika kwa wakati kama ilivyopangwa ili kukuza uchumi lakini ni jambo la muhimu unafuata masharti ya Cheti cha Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM) kilichotolewa na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC).

“Nimekuja hapa kukagua mradi huu wa reli ya kisasa na hapa nimekuja maalumu kwa ajili ya kukagua eneo la mazingira, sasa niwatake wengine wenye miradi kama hii kufuata masharti yaliyowekwa kwenye cheti cha mazingira,” alisema.

Aidha, Waziri Jafo alisema kuwa ni muhimu kushirikisha wataalamu kutoka taasisi mbalimbali ili waweze kutoa ushauri wa namna ya kuboresha maeneo mbalimbali ya miradi bila kuathiri mazingira.

“Mradi ukikamilika siku tunaona treni ya umeme inapita na mazingira yako salama na hapa mtu akija kupima mradi wetu kimataifa anaiona thamani ya mradi wa Tanzania ni mzuri na umejali mazingira, hilo ndilo jambo la msingi,” alisema.

Hata hivyo alisema kuna baadhi ya watu wakipata cheti cha mazingira wanakiweka hawasomi masharti yaliyowekwa na kuyafuata hivyo aliwataka kufuata masharti ya kila eneo.

Settings