Waziri Jafo aagiza marekebisho lambo lililochimbwa Mpwapwa

Apr, 08 2023

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe.Dkt.Selemani Jafo ameagiza kufanyika kwa marekebisho katika lambo lililochimbwa katika Kijiji cha Kazania Halmashauri ya Mpwapwa mkoani Dodoma ili liweze kuzalisha maji kwa kiwango kikubwa kama ilivyotarajiwa.

Ametoa agizo hilo alipofanya ziara ya kushtukiza katika kijiji hicho kukagua lambo hilo lililochimbwa kupitia Mradi wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi kwa Kutumia Mfumo Ikolojia Vijijini (EBARR) unaoratibiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais.

Dkt. Jafo ambaye alikuwa lambo hilo halijajaa maji inavyotakiwa pamoja na kunyesha kwa mvua katika siku kadhaa zilizopita akirejea ziara aliyofanya Desemba 22, 2022 ambapo alionesha wasiwasi wa namna lambo hilo lilivyokuwa likichimbwa.

Wakati wa ziara ile alionesha wasiwasi lisijae maji akisema japo sio mtaalamu alitoa ushauri kwa wataalamu wa Tume ya Umwagiliaji ambao ndio wanafanya usanifu wa malambo kuzingatia kujenga mifereji ili kujaza maji kwa haraka.

Ofisi ya Makamu wa Rais imetoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi hii ya mazingira na tume hiyo ndio inaelekeza maeneo sahihi ambayo uchimbaji wa malambo unaweza kufanyika lakini hapa tume mmetuangusha nilitegemea katika mvua hizi lingekuwa limejaa na hapa naona wananchi wanachota maji yenye rangi hii ya udongo na yangekuwa meupe kama yangekuwa yamejaa kwenye lambo,“ alisema.

Kutokana na hali hiyo amewaagiza wataalamu wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji kufanya marekebisho ya lambo ikiwemo kutengeneza mifereji ifikapo Juni 2023 ili maji yaweze kupita kwa urahisi tofauti na ilivyo sasa.

Waziri Jafo alisema maeneo mengi ya Dodoma yanakabiliwa na ukame kutokana na athari za mabadiliko ya tabianchi hivyo wananchi hawana budi kuendelea kupanda miti kwa wingi ili kukabiliana na hali hiyo.

Katika hatua nyingine Dkt. Jafo alielekeza ifikapo Mei 2023 kazi ya uchimbaji wa visima ili wananchi waepukane na adha ya ukosefu wa maji safi akisema kuwa dhamira ya Serikali ni kuona wananchi wananufaika. Alisema Ofisi ya Makamu wa Rais ni mtambuka hivyo inatekeleza miradi katika sekta mbalimbali zikiwemo Kilimo, Mifugo, Uvuvi na Maji

Kwa upande wake Katibu Tawala wa Wilaya ya Mpwapwa Bi.Sarah Komba aliishukuru Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kutekeleza mradi huo wilayani hapo na kusema wananchi wameupokea vizuri.

Alisema lambo hilo limejengwa kimkakati na kuwa wananchi litatunzwa na kutumika vizuri kama inavyotarajiwa ili liweze kuwanufaisha wananchi na kuondokana na adha ya uhaba wa maji unaowakabili.

Bi.Sarah aliahidi kuwa Serikali ya Wilaya itatekeleza maelekezo aliyotoa Waziri jafo na kuwa itasimamia kazi ya maboresho itakayofanyika.

Naye Diwani wa Kata ya Nghambi Richard Milimo alitoa wito kwa wataalamu kuzingatia ushauri aliotoa Waziri Jafo kuhusu kujenga mifereji ili kuongeza ujazo wa maji kuingia katika lambo hilo.

Mratibu wa Mradi wa EBARR Halmashauri ya Mpwapwa Bw. Aziz Bilu alisema uhaba wa mvua umechangia pia kutojaa kwa lambo hilo kwa wakati ambapo imenyesha kwa siku saba katika miezi minne.

Hivyo, mratibu huyo alisema wameyapokea maelekezo ya Mheshimiwa Waziri na kuahidi kuwa watafanya marekebisho katika lambo hilo ili liweze kujaa maji.

Settings