Serikali inatathmini athari za mafuriko

Apr, 07 2024

Serikali imesema inaendelea na kazi ya kutathmini athari za mafuriko kwenye maeneo yaliathiriwa na mvua ili kupata taarifa za uharibifu wa mazingira.

Imesema taarifa hiyo itasaidia kuona namna bora ya kushughulikia changamoto hiyo.

Kauli hiyo imetolewa bungeni leo na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Mhe. Khamis Hamza Khamis wakati akijibu swali la Mbunge wa Ngorongoro, Mhe. Emmanuel Sahangai.

Katika swali lake, Mbunge huyo ametaka kujua ni lini serikali itafanya tathimini ya uharibifu wa mazingira ya Mto Juhe Pinyinyi uliotokana na mafuriko-Ngorongoro.

Akijibu swali hilo…….amesema kutokana na uharibifu wa mazingira ya mito hiyo, Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro kwa kushirikiana na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira(NEMC) kanda ya Kaskazini inaendelea kufanya tathimini ya athari hizo.

“Taarifa za kina zikipatikana kuhusu athari za uharibifu wa mazingira uliotokana na mafuriko hayo, zitatusaidia serikali kuona namna bora ya kushughulikia changamoto hii.“

Akijibu swali la nyongeza la mbunge huyo kuhusu mpango wa dharula wa Serikali wa kudhibiti madhara yanayotokana na mafuriko, Naibu Waziri Khamis amesema jitihada zinaendelea kufanyika ili kuzuia madhara.

Amesema Serikali inawezesha ujenzi wa kuta za kingo za mito ili kupunguza kasi ya maji yasiendel kwenye makazi pamoja na kuruhusu usafishaji wa mito kwa kuondoa mchanga.

Settings