‘Ni kosa kuacha kufukia mashimo baada ya uchimbaji‘

Oct, 21 2023

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis amesema ni kosa kuacha bila kuyafukia mashimo yaliyotokana na uchimbaji wa makaa ya mawe na madini mengine.

Pia amewataka wenye magari yanayobeba makaa yam awe kuyafunika ili kuepusha vumbi linaloweza kusambaa na kusababisha madhara kiafya na mazingira kwa ujumla.

Ametoa kauli hiyo alipofanya kikao na uongozi wa Wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma wakati wa ziara ya kufuatilia utekelezaji wa Mradi wa Mradi wa Kuhifadhi Ardhi katika Bonde la Ziwa Nyasa unaoratibiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais.

Kutokana na changamoto hiyo Mhe. Khamis amewataka viongozi kusimamia maelekezo yaliyotolewa na Serikali kuhakikisha wamiliki wa migodi hiyo pamoja na kuwa wanawekeza lakini wanapaswa kujali mazingira.

“Nitoe wito kwa wawekezaji kwenye migodi ikiwemo ya makaa ya mawe wafuate sheria na taratibu za utunzaji na uhifadhi wa mazingira maana athari ni nyingi wanaharibu mazingira, wanaharibu nutrientsza udongo na hata njia wanazotumia katika uchimbaji baadhi yao si sahihi, Serikali inatumia fedha nyingi kuhakikisha sekta ya mazingira inaimarika,“ amesisitiza Naibu Waziri Khamis.

Amesema kuwa ni kweli Serikali inawathamini wawekezaji mbalimbali wakiwemo wa sekta ya madini lakini wanapaswa kufuata sheria ili kunusuru mazingira kwa maendeleo endelevu ya nchi.

Awali Mkuu wa Wilaya ya Mbinga Aziza Mangosongo amesema bado kuna changamoto ya wananchi kufanya shughuli za kibinadamu kando ya mito na kusababisha uharibifu wa mazingira.

Pia, amesema baadhi ya wenye migodi hukata miti kwa matumizi yao wakidai kuwa leseni ya uchimbaji inawapa kibali cha kutumia kila kitu wanachokikuta katika eneo walilopewa kufanya uwekezaji huo, hali inasavavisha uharibifu wa mazingira.

Settings