Makamu wa Rais auaga mwili wa aliyekuwa Mtumishi wa Ofisi yake

May, 01 2023

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango na Mkewe Mama Mbonimpaye Mpango leo tarehe 1 Mei 2023 katika Uwanja wa Ndege wa Dodoma wamewaongoza watumishi wa Ofisi ya Makamu wa Rais katika kuaga na kusindikiza mwili wa aliyekuwa Mtumishi wa Ofisi ya Makamu wa Rais Marehemu Emmanuel Majanja aliyefariki kwa ajali ya gari tarehe 28 Aprili 2023 eneo la Mbande mkoani Dodoma. Mwili huo umesafirishwa kuelekea Ukerewe mkoani Mwanza kwaajili ya mazishi.

Akiwafariji watumishi,ndugu, jamaa na marafiki wa Marehemu Emmanuel Majanja waliojitokeza Uwanja wa Ndege Dodoma, Makamu wa Rais Makamu wa Rais amemtaja marehemu Majanja kama mtu aliefanya kazi yake vema na kwa bidii kubwa enzi za uhai wake. Amesema ni vema kuendelea kuwafariji na kuwasaidia wafiwa ikiwemo wajane na watoto walioachwa na marehemu.

Makamu wa Rais ametoa wito kwa jamii kuona umuhimu wa kuacha wosia na kuhakikisha wajane na yatima wanalindwa na kutodhulumiwa mali pindi msiba unapotokea. Aidha amesema ni vema kuendelea kujifunza kuishi vema kwa kutengeneza marafiki wengi zaidi ya maadui na kutambua siku za kuishi duniani si nyingi.

Makamu wa Rais amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa faraja aliotoa kwa Ofisi ya Makamu wa Rais kufuatia ajali iliotokea ikiwemo kutoa ndege kwaajili ya kusafirisha miili ya waliofariki katika ajali hiyo. Pia amelishukuru Jeshi la Wananchi Tanzania kwa namna walivyoshiriki katika msiba huo.

Settings