Makamu wa Rais ateta na Naibu Waziri Mkuu wa Ethiopia Uswisi

Jan, 16 2024

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango amekutana na kufanya mazungumzo na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Ethiopia Mhe. Demeke Mekonnen Hassen, Mazungumzo yaliyofanyika kando ya Mkutano wa Jukwaa la Uchumi Duniani (WEF) unaofanyika Davos nchini Uswisi.

Mazungumzo hayo yamelenga kuimarisha ushirikiano baina ya Tanzania na Ethiopia katika masuala ya kiuchumi na diplomasia.

Katika hatua nyingine Makamu wa Rais amefanya mazungumzo na Mkurugenzi wa Taasisi ya Global Plastic Action Partnership Bi. Clemence Schidm. Katika mazungumzo hayo, Makamu wa Rais ameikaribisha taasisi hiyo kushirikiana na Tanzania katika kukabiliana na taka za plastiki ikiwemo kufanya tafiti zitakazowezesha kutambua aina ya taka za plastiki zinazopatikana kando ya bahari na maeneo ya nchi kavu ili kusaidia kuandaa mkakati wa kukabiliana na changamoto hizo.

Pia Makamu wa Rais ameikaribisha Taasisi hiyo kushirikiana na Tanzania katika kudhibiti taka za plastiki hususani Makao Makuu ya nchi Dodoma kwa kuanzisha miradi itakayowezesha katika uchakataji wa taka na utengenishaji wa taka za plastiki. Aidha amesema ni vema kuandaa jukwaa la kimataifa kuhusu uchakataji wa taka za plastiki ambalo litawezesha kuwakutanisha wakusanya taka wa ndani ya nchi na makampuni ya kimataifa ya ukusanyaji taka ili kujadili na kupata uzoefu kutoka katika makampuni hayo.

Makamu wa Rais yupo nchini Uswisi kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Mkutano wa Jukwaa la Uchumi Duniani unaofanyika katika mji wa Davos.

Settings