Makamu wa Rais akemea utupaji taka ovyo

Apr, 16 2023

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango ametoa wito kwa watanzania kuacha tabia ya kutupa taka ovyo katika maeneo mbalimbali wanayotumia hususani barabarani.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati akiwasalimu waumini wa Kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu Petro iliopo Swaswa jijini Dodoma mara baada ya kushiriki Ibada ya Jumapili katika kanisa hilo leo tarehe 16 Aprili 2023.

Amesema uwepo wa mvua zisizotabirika ni kutokana na uharibifu wa mazingira uliokwishafanyika hivyo kila mmoja aone umuhimu wa utunzaji mazingira mazuri ambayo nchi imejaaliwa na Mwenyezi Mungu.

Makamu wa Rais ametoa rai kwa waumini hao na watanzania kwa ujumla kuona umuhimu wa kupanda miti katika makazi yao ikiwemo miti ya matunda na kivuli pamoja na kuongeza jitihada katika usafi wa mazingira ili kukabiliana na athari zitokanazo na uharibufu wa mazingira zinazojitokeza hivi sasa.

Halikadhalika Makamu wa Rais amewakumbusha waumini juu ya kuzingatia maadili mema ya kitanzania katika malezi ya watoto na vijana pamoja na kutoa wito kwa wamiliki wa taasisi za kutolea elimu kujielekeza katika kusimamia maadili mema ya kitanzania katika maeneo yao.

Settings