Makamu wa Rais aiagiza Wizara ya Maji kupeleka maji Same

Mar, 21 2024

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango ameagiza uongozi wa Wizara ya Maji pamoja na watendaji wa Wizara hiyo kuhakikisha miji ya Same na Mwanga inapatiwa huduma ya maji safi na salama kupitia mradi wa Maji wa Same – Mwanga – Korogwe ifikapo mwezi juni mwaka huu 2024.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati alipotembelea chanzo cha mradi huo kilichopo eneo la Nyumba ya Mungu Wilaya ya Mwanga mkoani Kilimanjaro. Amewataka watendaji wa Wizara ya Maji kujipanga vizuri kuwasimamia wakandarasi kwa kufanya kazi usiku na mchana ili adhma na maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa juu ya mradi huo yaweze kutekelezwa.

Makamu wa Rais amesema wananchi wa maeneo hayo wamesubiri mradi huo kwa miaka 19 tangu ulipoahidiwa mara ya kwanza hivyo ni wakati wa kuhakikisha mradi huo unakamilika. Amemtaka Waziri wa Maji kutembelea mradi huo mara kwa mara ili kutambua changamoto na kuzitatua haraka iwezekanavyo.

Aidha Makamu wa Rais ameuagiza uongozi wa Mkoa wa Kilimanjaro kuhakikisha wanalinda mazingira na chanzo cha maji ya mradi huo ili kuwa endelevu.

Wakandarasi wa Mradi huo wameahidi kufikia malengo yaliyowekwa ya kuhakikisha mradi huo unakamilika ifikapo mwezi juni mwaka huu 2024.

Settings