Magereza waanza kutumia nishati safi ya kupikia

Jan, 26 2024

Jeshi la Magereza limeanza kusitisha matumizi ya kuni na mkaa na kuanza kutumia nishati safi ya kupikia ikiwa ni hatua ya kuunga mkono jitihada za Serikali za kupunguza ukataji wa miti.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Bi. Miriam Mmbaga akimwakilisha Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Hamad Yussuf Masauni katika zoezi la upandaji miti kuelekea Maadhimisho ya Miaka 60 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, lililofanyika leo Januari 26, 2024.

Akiwaongoza maafisa na askari wa jeshi hilo, Bi. Mmbaga amesema kuwa jeshi hilo ni mdau mkubwa utunzaji mazingira hivyo wizara hiyo imetenga fedha kwa ajili ya kuanza matumizi ya nishati safi.

Amebainisha kuwa Gereza la Mtwara, Keko na Ukonga ya jijini Dar es Salaam, Mpanda, Chuo cha TCTA na Shule ya Sekondari ya Bwawani zimeanza kutumia nishati safi ya kupikia akisema matarajio ni jeshi hilo kuachana kabisa na matumizi ya kuni na mkaa.

Aidha, Bi. Mmbaga amelipongeza Jeshi la Magereza kwa kuwa mstari wa mbele katika kutekeleza maelekezo ya Serikali ya kukijanisha Mji wa Dodoma kwa kupanda miti.

Sanjari na hayo amewaelekeza wakuu wa Magereza yote nchini kupanda miti ya miaka 60 na kuitunza ambayo pamoja na kuleta faida mbalimbali lakini pia itasaidia kuchagiza biashara ya kaboni.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais Bw. Abdallah Hassan Mitawi amesema zoezi la upandaji miti linafanyika kama kielelezo cha kushereheka maamuzi ya busara ya waasisi wa Muungano kwa kuziunganisha nchi hizi mbili na kuwa moja.

Amesema upandaji wa miti 60 na kuendelea ni kuonesha imani kuwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar utaendelea kudumu kwa miaka zaidi ya 60 mingine ijayo.

Bw. Mitawi amesema kuwa zoezi hilo la upandaji miti kuuunga mkono ‘Kampeni Kukijanisha Dodoma’ iliyoanzishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kulifanya Jiji la Dodoma kuwa la kijani.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Jabir Shekimweri ameshauri ajenda ya kupanda miti kupitia Jeshi la Magereza kuangaliwa katika jicho la kiuchumi kwa kuchangia katika biashara ya kaboni.

Amesema kuna umuhimu wa kutumia nguvu kazi iliyonayo jeshi hilo kwa kupanda miti kwa wingi katika maeneo yake ambayo itasaidia katika kunyonga hewa chafu na hivyo kuingiza mapato.

Zoezi hilo la upandaji wa miti limefanyika kuzunguuka Hospitali Kuu ya Kanda ya Kati ya Jeshi la Magereza iliyopo Veyula jijini Dodoma na linatarajiwa kuendelea Januari 27, 2024 eneo la Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).

Settings