Katibu Mkuu Maganga awataka wataalumu kuibua miradi ya mazingira

Jan, 26 2024

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Bi. Mary Maganga amewaasa wataalamu kuendelea kuibua na kuandika miradi mingine ili kutatua changamoto za mazingira nchini.

Ametoa rai hiyo wakati wa Kikao cha Kamati ya Uendeshaji wa Mradi wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi kwa kutumia Mifumo Ikolojia Vijijini (EBARR) kilichoketi jijini Dodoma.

Bi. Maganga ambaye ni mwenyekiti wa Kamati hiyo amesistiza umuhimu wa kusimamia miradi kwa ufanisi ili matokeo yake yaweze konekana na kuinufaisha jamii.

Halikadhalika amewasistiza wasimamizi wa mradi kuhakikisha wanakamilisha shughuli zilizopangwa kwa wakati ili kuepusha mradi kufika mwisho wa muda wake kabla ya shughuli kukamilika.

Bi. Maganga ni mwenyekiti Kamati hiyo inayoundwa na Makatibu Wakuu wa Wizara sita, Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar na mwakilishi wa Asasi za Kiraia (AZAKI).

Aidha, Kamati hiyo imekutana kwa ajili ya kupokea taarifa za utekelezaji wa mradi pamoja mapendekezo ya bajeti na mpango wa utekelezaji kwa mwaka 2024.

Katika kikao hicho Kamati ya Uendeshaji wa Mradi kilichohudhuriwa na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Dkt. Omar Dadi Shajak kimeidhinisha bajeti na mpango wa utekelezaji kwa mwaka 2024.

Itakumbukwa kuwa Mradi wa EBARR unatekelezwa katika wilaya za Mpwapwa (Dodoma), (Mvomero) Morogoro, Simanjiro (Manyara), Kishapu (Shinyanga) na kwa upande wa Zanzibar Wilaya ya Kaskazini ‘A‘ (Mkoa wa Kaskazini – Unguja).

Settings