Katibu Mkuu Maganga aishukuru GCF kwa ufadhili wa miradi

Jan, 10 2024

Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Bi. Mary Maganga ameushukuru Mfuko wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi (GCF) kwa kuendelea kufadhili miradi mbalimbali nchini.

Ametoa shukurani hizo alipokutana na kufanya mazungumzo na Ujumbe wa Sekretarieti ya Mfuko huo ukiongozwa na Meneja wa GCF Kanda ya Afrika Bi. Chihenyo Kangara katika ofisi ndogo ya Ofisi ya Makamu wa Rais jijini Dar es Salaam.

Miongoni mwa miradi inayofadhiliwa na GCF kwa sasa ni pamoja na Mradi wa Maji unaotekelezwa mkoani Simiyu, Mradi wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi mkoani Kigoma, Mradi wa Uandaaji wa Mpango Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi na Mradi wa Kilimo kupitia benki ya CRDB.

Pia, Katibu Mkuu Maganga amesisitiza kuhusu umuhimu wa Taasisi za Tanzania kupata idhibati chini ya Mfuko huo na ukamilishwaji wa mapendekezo ya miradi yaliyowasilishwa GCF Ili kuwezesha upatikanaji fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi hiyo kwa wakati.

Aidha, miradi iliyowasilishwa GCF inahusu Uchumi wa Buluu, Afya, Uzalishaji wa Umeme kwa kutumia joto ardhi, Mradi wa Mabasi ya Mwendo kasi na Mradi ya Maji.

Kwa upande wa kiongozi wa msafara wa GCF Bi. Chihenyo ameahidi kuhakikisha kuwa hakuna ucheleweshaji tena ktk maombi mengine.

Ameeleza kuwa kwa sasa wako kwenye mageuzi katika maeneo ya uongozi na mipango pamoja na taratibu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutembelea wadau ili kutoa huduma inayokubalika.

Settings