Dkt. Jafo apongeza uzingatiaji Sheria kiwanda cha nondo Mkuranga

Nov, 13 2023

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Dkt. Selemani Jafo amesema Serikali imeridhishwa na utekelezaji wa maelekezo yake ya utunzaji wa mazingira katika kiwanda cha nondo cha Lodhia kilichopo wilayani Mkuranga Mkoa wa Pwani.

Amesema hayo wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira ya kukagua utekelezaji wa maelekezo ya Serikali kuhusu utunzaji wa mazingira leo Novemba 13, 2023.

Kutokana na hali hiyo Dkt. Jafo ametoa wito kwa wawekezaji wengine wenye viwanda waige mfano huo kwa kutunza mazingira katika maeneo yao ili kulinda afya za wananchi.

Amesema katika ziara yake iliyopita kiwandani hapo alitoa maelekezo mbalimbali yakiwemo kutenga eneo la kuhifadhi chuma chakavu na kuhakikisha moshi hauathiri wananchi, ambayo yametekelezwa.

Amewataka wawekezaji wa viwanda kuzingatia Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004 kwa kuhakikisha moshi hausambai angani hali inayochangia ongezeko la joto.

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Anna Lupembe amesema kuwa utekelezaji wa maelekezo hayo ni matunda ya kazi nzuri ya usimamizi inayofanywa na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira.

Amewapongeza kwa kutoa elimu kwa wawekezaji ambapo wameweza kudhibiti uchafuzi wa mazingira na kelele kutokana na mitambo.

Aidha Mhe. Lupembe amepongeza juhudi za Serikali za kukuza sekta ya viwanda ambayo imechagiza ukuaji wa ajira kurahisisha upatikanaji wa bidhaa hizo za nondo.

Settings