Dkt. Jafo aingilia kati uchimbaji mawe kinyume cha utaratibu Dodoma

Mar, 14 2024

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Dkt. Selemani Jafo amelielekeza Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Jiji la Dodoma pamoja na Ofisi ya Madini Mkoa wa Dodoma kufanya tathmini na kumpa taarifa ya mazingira katika vilima vilivyopo katika jiji hilo.

Ametoa agizo hilo leo Machi 14, 2024 wakati wa ziara ya ukaguzi wa machimbo ya kokoto, katika Kata ya Iyumbu, jijini Dodoma ambako wananchi huchimba mawe kwa ajili ya kuponda kokoto.

Katika maelekezo hayo amewataka watendaji hao kwani kutoa ushauri wa nini kifanyike kunusuru hali hiyo kwani watu wengi huchimba maeneo hayo bila maelekezo.

Dkt. Jafo amefafanua kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Mazingira ibara ya 58 (2 D) inatoa maelekezo ya kulinda huku akitahadharisha kutoweka kwa vilima hivyo.

“Mnaelewa Sheria ya Mazingira ndio sheria mama, hivyo natoa maelekezo. Kwanza mtambue sijaridhika na hii hivyo nawapa wiki mbili mje na ripoti ili tuone namna ya kuyahifadhi na kuyatangaza maeneo haya,” amesema Dkt. Jafo.

Pia, Dkt. Jafo amesisitiza miji duniani ambayo imefanya vyema katika mazingira hivyo na hapa nchini kila mmoja anatakiwa kuchukua hatua ya kulinda mazingira.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Iyumbu, Elias Richard amemwomba Waziri Jafo wawahusishe wakati wa kufanya maamuzi ili kutoa muelekeo wa kusimamia maeneo hayo kwa kuwa hajaridhika na hali ya mazingira katika kata hiyo.

“Tayari hili jambo nimeliwasilisha kwenye Baraza la Madiwani na ninashukuru kwa ujio wako sababu wengi wanafanya kazi wakiwa ofisini na si kutembelea eneo hivyo nikuombe tushirikiane katika hili ili kulinda mazingira yetu,” amesema.

Settings