Nchi zilizoendelea zaombwa kusaidia katika kuhimili mabadiliko ya tabianchi

May, 18 2021

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Hamad Hassan Chande ametoa wito kwa nchi zilizoendelea zikiwemo za Umoja wa Ulaya (EU) kuendelea kuzisaidia nchi zinazoendelea katika kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi.

Alisema hayo wakati akizindua Maonesho ya Mabadiliko ya Tabianchi Mei 18, 2021 katika Ukumbi wa Makumbusho ya Taifa jijini Dar es Saalam yaliyoandaliwa na EU kwa kushirikiana na Tanzania.

Chande alisema kuwa athari za mabadiliko ya tabianchi ni kubwa na zimeendelea kuathiri kwa kiwango kikubwa nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania.

“Serikali inakamilisha Mkakati wa Taifa wa kukabiliana na athari za Mabadiliko ya Tabianchi wa Mwaka 2021 – 2026 ambao pamoja na mambo mengine unalenga kuimarisha uwezo wa kitasisi katika kukabiliana na changamoto zitokanazo na mabadiliko ya Tabianchi”, alisema.

Pia Naibu Waziri huyo alihimiza EU kuendelea kushirikiana na Tanzania katika masuala mbalimbali ya hifadhi ya mazingira ikiwa ni pamoja na kuhamasisha matumizi ya nishati jadidifu; usimamizi wa taka na kufanya tafiti mbalimbali kwa ajili ya maendeleo endelevu.

Kwa upande wake Balozi wa EU nchini Mhe. Manifredo Fanti alisema kuwa Umoja huo utaendelea kushirikiana na Tanzania katika masuala mbalimbali hususan hifadhi ya mazingira na mabadiliko ya Tabianchi.

“Tumepanga kutumia asilimia 25 ya Bajeti yetu ya awamu hii kwa ajili ya kuisaidia Tanzania katika kusimamia masuala ya hifadhi ya mazingira na mabadiliko ya tabianchi”, alisema Balozi Fanti.

Maonesho hayo yameshirikisha wadau mbalimbali wakiwemo mabalozi kutoka baadhi ya nchi za Umoja wa Ulaya, mashirika ya Umoja wa Mataifa na asasi za kiraia.

Mabadiliko ya tabianchi yana athari kubwa zikiwemo:mmomonyoko wa udongo, ongezeko la kiwango cha maji ya bahari na athari zinginezo ambazo zimeathiri maisha ya watu.

Settings