Jiji la Tanga kinara wa usafi wa mazingira

Apr, 15 2024
Jiji la Tanga limetajwa kuwa mfano wa kuigwa nchini katika suala la usafi wa mazingira hali inayosaidia wananchi katika kujikinga na magonjwa ya mlipuko. Akizungumza wakati wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2024 mkoani Tanga Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu amesema jiji hilo limefanikiwa kwa asilimia kubwa katika utunzaji wa mazingira. Mhe. Ummy ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Tanga Mjini amesema wananchi wa wamekuwa mwitikio mkubwa katika kufanya usafi pamoja kutoka na uongozi kuweka mpango mzuri wa ukusanyaji wa taka ndani ya jiji na kuzipeleka katika dampo la kisasa lililojengwa na Halmashauri ya Jiji hilo. “Hadi sasa na kwa mujibu wa taarifa zangu za Wizara ya Afya, Jiji la Tanga ndio jiji pekee ambalo halijapata ugonjwa wa kipindupindu na hii ni sababu ya kazi kubwa inayofanywa na viongozi katika kusimamia masuala la usafi wa mazingira,” “Nashukuru watu wa Tanga kwa kuendelea kusimamia mazingira na kuliweka Jiji safi pamoja na mazingira ya mji kuwa katika mazingira mazuri hivyo tuzidi kuweka mji wetu safi muda wote,” amesema Mhe. Ummy. Kwa upande wake Afisa Mazingira wa Halmashaurii ya Jiji la Tanga Bi. Zamoyoni Mohamed amesema katika suala la udhibi wa taka wilaya imetoa ajira za muda 152 kwa ajili ya kufanya usafi wa mazingira na kuondoa taka. “Wananchi huhamasishwa kuishi katika mazingira yaliyo safi wakati wote na pia kushiriki kwa pamoja kufanya usafi kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi. “Taka zinazozalishwa zinaondolewa na kudhiibitiwa kwenye Dampo rasmi lililopo Mpirani, Aidha, katika udhibiti taka ngumu, wadau mbalimbali wanaofanya shughuli za urejezaji wameweza kutambuliwa na kupewa ushirikiano. Bi. Zamoyoni ameongeza kuwa takribani tani 176 za taka hudhibitiwa kwa siku na kulifanya jiji lote kuwa safi muda wote. Kaulimbiu ya Mbio za Mwenge Kitaifa 2024 inasema “Tunza Mazingira na Shiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa Ujenzi wa Taifa Endelevu.”
Settings