Waziri Jafo ahamasisha wanafunzi kufanya tafiti za mazingira

Aug, 05 2021

Waziri Jafo ahamasisha wanafunzi kufanya tafiti za mazingira

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Selemani Jafo ametoa rai kwa wanafunzi wa sekondari na vyuo kufanya tafiti zitakazosaidia kupambana na changamoto za kimazingira.

Jafo ametoa rai hiyo leo Agosti 5, 2021 alipotembelea Mradi wa Ustawishaji miche kwa kutumia vyungu unaotumia maji kidogo uliobuniwa na wanafunzi wa Shule ya Sekondari St. Crolus katika Manispaa ya Singida.

Aliwapongeza wanafunzi hao wanaosoma kidato cha kwanza katika shule hiyo kwa ubunifu wa mradi huo na kusema kuwa ni mojawapo ya mbinu za kuhifadhi mazingira.

“Nimefurahishwa sana wanafunzi hawa na hii inanipa faraja kubwa kwani vijana hawa wakimaliza kidato cha nne watakuwa watu mahiri kabisa na ndio maana natoa wito kwa shule zingine kufanya tafiti zao kuhusu mazingira tupate kutatua changamoto za mazingira,” alisema Jafo.

Aidha, waziri huyo aliwapongeza wanafunzi hao kwa kuwa mradi huo unatumia maji kigogo katika kustawisha miche ya miti hatua inayosaidia kupunguza umwagiliaji wa kila siku.

Pia alisema mradi huo unasaidia kupunguza uchafuzi wa mazingira kwa kuwa hutumia uchafu zikiwemo ndoo kwa ajili ya kupandia miche ambazo kama zingeachwa zingeweza kuzagaa katika mazingira.

Katika hatua nyingine Waziri Jafo aliwataka wataalamu wa kilimo katika Halmashauri kuzunguka katika vijana wanaobuni miradi kama hiyo na kuwapa elimu ya matumizi ya mbolea kwa usahihi ili miche inayostawishwa iweze kukua.

Kwa upande wake Msimamizi wa Mradi huo, Mwalimu Yesaya Bendera alisema matarajio yao katika utafiti huo ni kupata majibu ambayo yatasaidia kuifanya Singida na nchi kwa ujumla kuwa ya kijani.

Mwalimu Bendera alisema kuwa kwa kutumia mbinu hiyo kutapunguza adha kubwa ya kuchota maji kwa wingi na kumwagilia miche na badala yake watatumia maji kdogo.

Aliongeza kuwa katika utafiti waliofanya Januari 2021 katika maeneo mbalimbali mjini Singida asilimia kubwa ya waliohojiwa walilalamika kutumia muda mrefu kuchota maji kwa ajili ya kumwagilia badala ya kufanya shughuli za uzalishaji, hivyo waliamua kubuni mradi huo.

Settings