Jafo aridhishwa uzingatiji wa maelekezo yake dampo la Chidaya, mabwawa ya majitaka DUWASA

Sep, 03 2021

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Selemani Jafo amefanya ziara ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa maelekezo aliyoyatoa miezi sita iliyopita katika dampo la Chidaya na mabwawa ya majitaka eneo la UDOM na Hospitali ya Benjamin Mkapa.

Katika ziara hiyo ameonesha kuridhishwa na utekelezaji wa maelekezo hayo aliyotoa na kutoa rai kwa watendaji wengine wa mamlaka za maji kuhakikisha wanasimamia vyema mifumo ya majitaka ili kulinda wananchi pamoja na mazingira.

Jafo aliipongeza Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira (DUWASA) na Halamshauri ya Jiji la Dodoma kwa kusimamia vyema mabwawa ya majitaka na dampo la taka ngumu na majitaka.

Alisema kuwa awali katika ziara yake ya kushtukiza Aprili 2021 alikuta hali isiyoridhisha katika miundombinu hiyo na hivyo kutoa maelekezo kwa Mkurugenzi wa Mamlaka hiyo na Mkurugenzi wa Jiji kuifanyia maboresho ili kulinda mazingira.

“Nimetembelea madampo mbalimbali ndani ya Tanzania likiwemo la Moshi, Arusha mpaka kule Kigoma na maeneo mengine lakini nilikuta hapa changamoto ya usimamizi usioridhisha hali ambayo endapo mvua ingenyesha yangetirirka kwenye makazi ya watu na kuleta athari za kiafya, sasa leo nimekuja hapa kufuatilia utekelezaji wa maelekezo hayo nimekuta mmetekeleza mmejenga ukuta ambao utasaidia kuzuia majitaka haya yasitiririke na kuleta athari kwa watu na si watu tu hata kwa viumbe,” alisema Jafo akiwa katika dampo la Chidaya.

Waziri Jafo aliwataka wasimamizi wa mradi huo wa dampo kuhakikisha ukuta waliojenga unadumu kwa muda mrefu ili wananchi wa Dodoma waendeele kuwa salama bila kuathiriwa na majitaka ambayo yangeweza kutiririka wakati wa mvua.

Pia Waziri Jafo aliwataka wasimamizi hao kulitumia vizuri dampo hilo na kuhakikisha taka zote zinazotupwa hapo zinashindiliwa vizuri ili zisisambae ovyo na kuleta uchafuzi wa mazingira.

Kwa upande Mkurugenzi wa DUWASA, Mhandisi Aron Joseph alimshukuru Waziri kwa kutembelea mradi huo mara kwa mara na kutoa maelekezo yake ambayo wameyatekeleza na hivyo hivyo hali ya mabwawa kuridhisha.

Meneja wa Kanda wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) alisema mawasiliano ya mara kwa mara kati ya Baraza hilo na DUWASA yamefanikisha utekelezaji wa maelekezo hayo.

Akitoa taarifa kuhusu utekelezaji wa maelezo ya awali, Meneja wa Dampo la Chidaya, Bw. John Kiwanga alisema mara baada ya kupokea maelekezo ya Waziri Jafo kupitia kwa Mkurugenzi wa Jiji waliyanfanyia kazi mara moja na kujenga ukuta huu.

“Kama unavyoona mheshimwa waziri hapa tumejenga ukuta huu kwa matofali ya kawaida tu na hatua hii itasaidia sana kuzuia majitaka kutoka katika dampo hili kutotoka nje na kuchafua vyanzo vya maji,” alisema Kiwanga.

Settings