​‘Ipo haja ya kuchukua hatua kukabili changamoto ya mabadiliko ya tabianchi’

Mar, 03 2021

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Mhandisi, Joseph Malongo amesema kuna haja ya kuchukua hatua za pamoja katika ngazi ya kitaifa, kimataifa na kikanda ili kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi.

Mhandisi Malongo amesema hayo leo mjini Morogoro katika hotuba ya ufunguzi wa Kongamano la Taifa la Wadau kukusu ukamilishaji wa mapitio ya Mkakati wa Taifa wa Mabadiiko ya Tabianchi (2012-2018) iliyosomwa kwa niaba yake na Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Mazingira Ofisi ya Makamu wa Rais, Catherine Bamwenzaki.

Alisema kuwa wadau wa maendeleo kutoka sekta binafsi, vyuo vikuu wanapaswa kushirikiana na Serikali katika hatua inazochukua katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

“Kuongezeka kwa joto duniani husababisha hali ya hewa kubadilika kila wakati na hii ni kutokana na shughuli za asili na pia mabadiliko haya yote yana athari kubwa kwa maisha ya watu na mifumo yetu ya ikolojia,” alitahadharisha.

Aidha, Mhandisi Malongo alibainisha kuwa athari za mabadiliko ya tabianchi zimeonekana katika sekta mbalimbali za kiuchumi zikiwemo maji, nishati, kilimo na usalama wa chakula, mifugo, miundombinu, makazi ya watu, afya ya binadamu na mifumo ya ikolojia.

Kwa mujibu wa utafiti kuhusu Uchumi wa mabadiliko ya hali ya hewa kwa Tanzania uliofanywa mwaka 2010, ilikadiriwa kuwa mabadiliko ya hali ya hewa ya baadaye yanaweza kuwa mabaya zaidi na kusababisha gharama kubwa za kiuchumi kwa nchi.

Utafiti huo ulibainisha kuwa mabadiliko ya sasa ya hali ya hewa tayari yanagharimu Tanzania karibu asilimia 1 ya Pato la Taifa kila mwaka na inaweza kuongezeka hadi asilimia 2 ifikapo mwaka 2030. Pia watu takriban milioni 0.3 hadi milioni 1.6 watakuwa hatarini kuathiriwa na kuongezeka kwa usawa wa bahari ifikapo mwaka 2030.

Kongamano hilo limeandaliwa na Ofisi ya Makamu wa Rais kwa ushirikiano na Taasisi ya Uongozi (Uongozi Institute) na kuhudhuriwa na wadau kutoka Wizara za kisekta, Taasisi za kiserikali, taasisi binafsi, asasi za kiraia, taasisi za kifedha na wataalamu wa mazingira kutoka Mikoa mbalimbali.

Settings