Waziri Zungu: Bomba la mafuta Afrika Mashariki salama kwa mazingira

Feb, 07 2020

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Mussa Azzan Zungu hii leo ameshuhudia makabidhiano ya Cheti cha tathmini ya athari kwa mazingira kwa mradi wa bomba la kusafirisha mafuta ghafi la afrika mashariki ikiwa ni hitimisho la ripoti ya Tathmini ya mazingira kwa Mradi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima hadi Bandari ya Tanga.

Amesema mradi huo ni wa bomba lenye urefu wa km1443 kutoka Uganda Wilaya ya Hoima hadi eneo la Chongoleani katika bandari ya Tanga na kwa upande wa Tanzania pekee bomba lina urefu wakilomita1114 ambao ni asilimia zaidi ya 80 zitakazopita katika mikoa Minane (8) na Wilaya 24 nchini “Furaha yangu inatokana na uhalisia kwamba sehemu kubwa ya mradi na vituo viko Tanzania na NEMC wameweza kufanya kazi hii na kumaliza kwa wakati, ambapo kwa upande wa Uganda bado wako kwenye hatua za mwisho. Natumaini hafla hii itawahimiza watendaji na Mamlaka za wenzetu kuweza kukamilisha tathmini hizi za Mazingira kwa wakati Zungu alisisitiza.

Hafla ya kukabidhi Cheti cha Tahtmini ya Mazingira kwa Mradi wa EACOP, ni Ushahidi wa Serikali kuridhia kuwa Mradi huu utahakikisha kwamba masuala ya kiuchumi, kijamii, mazingira, afya na usalama yanashughulikiwa wakati wote wa kipindi cha kupanga, kujenga na uendeshaji wa shughuli za bomba. “Ili kupunguza athari kwa mazingira na jamii njia litakapopita bomba vituo vitawekwa na kuendeshwa kwa umakini ili kupunguza athari yoyote ya kimazingira na kiikolojia Zungu aliainisha.

Waziri Zungu amesema kuwa kazi ya Serikali kupitia NEMC haiishii kutoa Cheti tu, bali kuendelea kufuatilia na kutathmini utekelezaji wake kulingana na masharti ya Cheti kilichotolewa.

Kwa upande mwingine Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani amesema kuwa hatua tano za awali zimekamilika katika utekelezaji wa mradi huo ikiwa ni pamoja na upakatikanaji wa eneo la kujenga matenki manne yenye uwezo wa kuhifadhi lita laki 2.5, kulipa fidia kwa wakazi wa eneo litakalohusika na mradi huo, tafiti za kijiolojia na fizikia na tathmini ya fidia kwa watakaopisha eneo katika korido ambayo itapita katika mikoa 8 na wilaya 24.

Settings