Waziri Zungu akagua bwawa la kuhifadhi tope sumu mgodi wa Barrick

May, 22 2020

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Mussa Azzan Zungu hii leo amekagua bwawa la kuhifadhia tope sumu katika Mgodi wa Dhahabu wa Barrick North Mara.

Waziri Zungu ameambatana na Waziri wa Madini Mhe. Dotto Biteko, Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Angela Mabula, Mwenyekiti wa Bodi ya NEMC Prof. Esinati Chaggu pamoja na watendaji wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC). Wakati wa ukaguzi huo Waziri Zungu amewashauri watendaji wa Barrick North Mara pamoja na bodi yao kuchagua teknolojia rafiki kwa mazingira na uchumi hasa katika kutibu maji yenye sumu yanayozalishwa na mgodi huo wa dhahabu.

Akizungumza na wananchi wa Nyamongo Waziri Zungu amewahakikishia ufuatiliaji wa sheria na taratibu za mazingira "Usalama wa Maji taka tumejiridhisha upo, na kwa kila kipindi tunafanya ukaguzi kuhakikisha maji taka haya hayaathiri wananchi waliouzunguka mgodi huu." Amesema Mhe. Zungu.

Aidha Mkurugenzi wa NEMC, Dkt. Samuel Gwamaka amesema wanafanyia kazi malalamiko ya wananchi wanaozunguka Migodi sambamba na kukagua iwapo taratibu za mazingira zinafuatwa katika migodi yote nchini "Barrick North Mara ni miongoni mwa migodi tunayofuatilia kuhakikisha uendeshaji wake hauleti madhara kwenye mazingira na wananchi wa maeneo ya jirani" Dkt Gwamaka

Hata hivyo serikali kwa kushirikiana na mamlaka mbalimbali imeendelea kuhakikisha kunakuwepo na mazingira rafiki kwa wenye migodi, wachimbaji pamoja na wananchi wanaoizunguka migodi hiyo.

Settings