Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mhandisi Hamadi Yussuf Masauni amesema Waandishi wa Habari wana wajibu mkubwa katika kusimamia uwepo wa taarifa zinazojenga Muungano na kuondoa upotoshaji unaoweza kusababisha mgawanyiko.
Mhe. Masauni amesema vyombo vya habari vina umuhimu wa kuhakikisha taarifa zinazochapishwa ni sahihi, zenye vyanzo vya kuaminika, kuandaa mijadala yenye tija, isiyo na jazba wala kuchochea mgawanyiko, kuangazia mafanikio ya Muungano badala ya kusubiri tu changamoto.
Ameyasema hayo Disemba 23, 2025 wakati akifungua Semina ya Wahariri wa Vyombo vya Habari jijini Dar es Salaam na kuongeza kuwa kwa kuwataka kutoa elimu kwa umma kuhusu masuala ya kikatiba, historia, na faida za Muungano pamoja na kutoa jukwaa la uwiano, linalosikiliza sauti zote bila kujenga uadui.
“Wahariri wa Vyombo vya Habari, kufuatilia kwa makini mada zitakazotolewa na wabobezi wetu wa masuala ya Muungano ili zitujengee weledi katika uandishi wa taarifa zinazohusu Muungano kwa maslahi mapana ya Taifa letu na mustakabali wa Muungano wetu adimu na adhimu”
“Mkakati huo unalenga kuhakikisha kizazi kipya kinatambua thamani ya urithi huo wa kihistoria, huku hatua kali za kisheria zikitajwa dhidi ya watu wanaojihusisha na hujuma au uharibifu wa misingi ya Muungano.
Amesema Ofisi imeandaa programu maalum zitakazokuwa vivutio kwa vijana, ikiwemo michezo na sanaa, ili kujifunza historia ya nchi yao. Pia, kutakuwa na utaratibu wa wanafunzi kutembelea maeneo ya kihistoria na kuanzishwa kwa chaneli mahususi itakayozungumzia masuala ya Muungano pekee.
Aliongeza kuwa ukosefu wa uelewa miongoni mwa vijana ni changamoto inayopaswa kutatuliwa ili waweze kuenzi misingi ya nchi bila kuyumbishwa na mabadiliko ya teknolojia au upotoshaji wa mitandaoni.