Waziri Jafo: Wadau wa maendeleo tushiriki kudumisha Muungano

Jun, 22 2022

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungana na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemanai Jafo ametoa wito kwa wadau wa maendeleo kuunga mkono juhudi za Serikali za kudumisha Muungano kwa kutoa elimu kwa wananchi kuhusu faida za zake.

Pia amesema Ofisi hiyo mbali ya kuandaa kitabu cha Historia ya Muungano pia, katika mwaka ujao wa fedha imetenga bajeti kwa ajili ya kuelimisha Watanzania ili wapate elimu ya kutosha kuhusu masuala ya Muungano.

Dkt. Jafo amesema hayo wakati akifungua Warsha ya Uratibu wa Muungano katika kuimarisha Uchumi wa Taifa jijini Dodoma iliyoshirikisha washiriki wa taasisi mbalimbali za Serikali zote mbili.

“Wapo baadhi ya watu hawaufahamu vizuri Muungano na pengine hata katika ofisi zetu kuna wengine hawafamu Muungano, wengine hadai wanastaafu wanaweza wasiufahamu Muungano hivyo tunatumia warsha hizi kutoa elimu,” alisema.

Akifunga warsha hiyo, Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Chilo aliwahimiza wadau kuhusu umuhimu wa kuimarisha Muungano kwa kuzungumzia fursa za kiuchumi.

Alisema hivi sasa kuna shughuli nyingi za kiuwekezaji na biashara zinazofanyika pande zote mbili za Muungano lakini hazifahamiki kwa wananchi hivyo ni wajibu wetu kuzunguzmia faida hizo.

“Muungano wetu ni fursa katika kuimarisha ukuaji wa uchumi wa Taifa letu na fursa hizo zinapatikana tu endapo shughuli za uratibu wa Muungano zitaendeshwa kwa ufasaha na kwa haraka na ziwe chachu ya upatikanaji wa taarifa za uhakika kuhusu hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali zote mbili katika nyanja za kiuchumi, kijamii na kisiasa,” alisema Chilo.

Naibu waziri huyo alitoa rai kuwa uratibu shughuli za Muungano ujikite zaidi katika kuhakikisha wadau wote muhimu wanashirikishwa kwa kupata taarifa kuhusu masuala muhimu ya Muungano.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Ofisi ya Makamu wa Rais Bw. Abdallah Hassan Mitawi alisema Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni wa kipekee kwasababu hatujamwaga damu katika kuungana.

Alisema tofauti na muungano wa zingine ulimwenguni, Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ulioasisiwa na Hayati Mwalimu Julius Nyerere na Hayati Shekhe Abeid Aman Karume unaendelea kudumu hadi sasa.

Akiendelea kuzungumza katika warsha hiyo, Bw. Mitawi aliongeza kwa kusema kuwa Muungano huu ni wa kipekee kwa kuwa umejengeka katika misingi ya kiundugu zaidi na hivyo kuufanya uwe imara.

Naye Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Kikuu cha Afya Muhimbili (MUHAS) Dkt. Harrison Mwakyembe aliwataka Watanzania kuuenzi Muungano kwa kuwa ndio utambulisho wetu ulimwenguni.

Dkt. Mwakyembe ambaye aliongoza timu ya uandishi wa kitabu cha Historia ya Muungano alisema kuwa Muungano ni alama ya Umoja wa Afrika hivyo hatuna budi kuhakikisha unaendelea kuwa imara zaidi.

Alisema yameonekana mafanikio mengi zaidi katika sekta mbalimbali ikiwemo ya elimu na uchumi mara baada ya kufanyika Muungano ukilinganisha na kipindi cha nyuma kabla ya Tanganyika na Zanzibar kuungana.

Settings