Tanzania yaandaa mpango wa kukabili uharibifu wa mazingira

Sep, 22 2022

Tanzania imeandaa mpango maalum unaoongoza namna ya kukabiliana na athari za uharibifu wa mazingira kulingana na ukubwa wa athari hizo katika kila eneo nchini.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula wakati akishiriki Mkutano wa Mawaziri kuhusu Mazingira na Maendeleo ulioandaliwa na Uingereza na Rwanda na kufanyika jijini New York tarehe 20 Septemba, 2022 ikiwa ni mkutano wa pembezoni wakati huu wa Mkutano wa 77 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (UNGA)

Balozi Mulamula alisema mpango huo umepangwa kulingana na ukubwa wa nchi na utofauti wa hali ya hewa katika kila eneo, misimu ya mvua, upepo, kiwango cha joto na shughuli za kijamii na kiuchumi katika eneo husika.

Ameongeza kuwa kupitia mpango huo changamoto 12 zinazotokana na uharibifu wa mazingira za uharibifu wa ardhi, ukataji miti, upotevu wa viumbe hai, mabadiliko ya hali ya hewa, uharibifu wa vyanzo vya maji na uharibifu wa fukwe na viumbe vya majini.

Alitaja changamoto zingine kuwa ni usimamizi wa taka, uchafuzi wa hewa na uvamizi wa viumbe yamebainishwa na hivyo yataisaidia nchi kuchukua njia stahiki kukabiliana nayo na kuyatafutia afua zake kikamilifu.

Pamoja na viongozi mbalimbali Mkutano huo umehudhuriwa na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Bi. Mary Maganga.

Settings