Sima: Serikali imeboresha Kanuni za Usimamizi Elekezi wa Mazingira

Feb, 01 2020

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mussa Sima amesema Serikali imeboresha Kanuni za Usimamizi Elekezi wa Mazingira ili kurahisisha na kuharakisha utoaji wa vibali vya tathmini ya mazingira.

Sima ametoa kauli hiyo jana bungeni jijini Dodoma wakati akichangia taarifa ya Kamati ya Viwanda, Biashara na Viwanda ya kipindi cha Julai hadi Desemba 2019 ambayo pamoja na mambo mengine ilizungumzia urasimu wa kutoa vibali

Alisema kuwa kupitia maboresho hayo sasa wataalamu hao wanaotambuliwa na Baraza la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) sasa utendaji kazi wao utaboreka kwakuwa kipengele cha kanuni hizo kitawabana wafanyde kazi kwa ueledi zaidi.

“Hili jambo tumelichukua kama lilivyo ili sasa twende tukakae na wataalamu wetu tukaweke njia sahihi kuondoa urasimu na tunatambua tumebadilisha kanuni lakini pia tunatambua katika suala la vibali leo tunatoa vibali vya muda mfupi ndani ya siku saba mtu anapata kibali wakati anasubiri kibali cha tatmnini ya mazingira ambacho kinachukua muda mrefu na ndio maana inawezekana wawekezaji wanaona kama kuna urasimu,” alisema.

Kwa upande mwingine kuhusu udhibiti wa biashara ya vyuma chakavu Naibu waziri aliwaondoa hofu wafanyabishara wa vyuma chakavu kuwa Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana na Wizara za Fedha na Mipango, Viwanda na Biashara pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama kuhakikisha tunalinda miundombinu isiharibiwe.

Hata hivyo Naibu Waziri Sima alikiri kuwa ipo changamoto ya uelewa mdogo wa masuala ya mazingira miongoni mwa baadhi ya wananchi ambapo alisema Ofisi hiyo imeendelea kutoa elimu kwa umma kupitia vyombo vya habari na semina ili kulipa uelewa kundi hilo la watu.

Settings