Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yadhamiria kuwapa stahiki zao wananchi wake

Mar, 09 2022

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla ametoa kauli hiyo katika hafla fupi ya kukabidhi Hundi ya fidia kwa wananchi wa eneo la Red Zone Tunguu hafla iliyofanyika Vuga Mjini Zanzibar.

Amesema katika kadhia iliyokuwa ikiwakabili wananchi hao Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya awamu ya nane kwa mashirikiano na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya awamu ya sita zimeamua kulisimamia jambo hilo ili wananchi hao walipwe fidia hiyo kwa mujibu wa Tathmini iliyofanywa na vyombo husika.

Aidha mhe. Hemed amewapongeza wananchi hao kwa uvumilivu wao na kueleza kuwa hatua hiyo inaonesha uungwana na uelewa waliokuwa nao na Imani kwa Serikali katika kipindi chote ambacho Serikali ilikuwa ikilisimamia jambo hilo.

Sambamba na hayo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ametumia fursa hiyo kuwataka wananchi hao kutoa taarifa sehemu husika iwapo itatokea miongoni mwao hajaingiziwa fedha ili Taasisi husika ichukue hatua za haraka.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi Ndugu Thabit Idarous Faina ameeleza kuwa miongoni mwa hatua zilizochukuliwa na Serikali katika kumaliza jambo hilo ni pamoja na ushirikishwaji wa Taasisi mbali mbali ikiwemp Ofisi ya Mthamini Mkuu wa Serikali .

Nae Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano Ndugu Abdallah Hassan Mitawi amemueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kuwa zoezi la kulipa fidia ni la muda ambapo hatua kadhaa zilichukuliwa kwa lengo la kumaliza malipo kwa wananchi ili kuweza kumaliza zoezi hilo.

Akitoa shukurani kwa Niaba ya wananchi wenzake Ndugu Muhamed Suleiman Khamis amezishukuru Serikali zote mbili kwa kuweza kumaliza kwa zoezi hilo hatua ambayo inaonesha namna Serikali zinavyowajali wananchi wake.

Nae Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja Mhe. Rashid Hadid amewapongeza wananchi hao kwa uvumilivu pamoja na kuendeleza Amani na utulivu kipindi chote wakati wakisubiri zoezi hilo kukamilika.

Zaidi ya Shilingi Bilioni 2 zimekabidhiwa wananchi waliohamishwa eneo la Red Zone Tunguu kupisha ujenzi wa Makazi ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania , ikiwa ni fidia kwa wenye maeneo hayo.

Settings