Naibu Waziri Chande atembelea dampo la kisasa la Manispaa ya Moshi

Sep, 22 2021

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Hamad Hassan Chande ametembela dampo la kisasa la Manispaa ya Moshi mkoani Kilmanjaro na kujionea uzalishaji wa mbolea kutokana na taka.

Akiwa katika ziara kwenye dampo hilo kwa ajili ya kukagua shughuli za utunzaji wa mazingira, Mhe. Chande alitoa wito kwa manispaa hiyo kuongeza wigo wa ukusanyaji taka ili kukidhi mahitaji ya soko la mbolea.

Pia, Naibu Waziri Chande aliongeza kwa kutoa wito kwa uongozi wa Manispaa ya Moshi kuwa na mpango wa kukusanya taka katika wilaya nyingine au mikoa mingine kama Arusha na Manyara ili kuzalisha mbolea itakayokidhi soko kubwa Zaidi.

Alisema ameridhishwa na kiwanda hicho cha mbolea kilichopo kwenye dampo hilo na kuwa ni hatua nzuri ambayo inasaidia katika usafi wa mazingira lakini pia inatoa fursa za ajira kwa wanaokusanya taka.

“Kiukweli katika dampo hili la kisasa Manispaa ya Moshi ina mipango mizuri kwani tumeona taka zile zinageuka na kuwa ni mali ambapo wanazalisha mboji yaani mbolea ambayo inahitajika sana kwa jamii yetu hasa wakulima,” alisema.

Kwa upande wake Afisa Mazingira ambaye pia ni Meneja wa Mradi wa uzalishaji wa mbolea, David Kimaro alikiri kuwepo kwa mahitaji makubwa ya soko la mbolea na kuahidi kutanua wigo wa ukusanyaji taka.

“Hadi kufikia sasa tumeweza kuzalisha tani karibia 54 za mbolea na tumeuza kwa mfano leo hii tuna oda ya tani 25 na tutazipaki leo kusafisha hadi Dar es Salaam, tuna wateja wengi ambao ni wakulima kutoka meeno mbalimbali kwa hiyo tunazidiwa na wateja,” alisema Kimario.

Settings