Makamu wa Rais Dkt. Mpango afungua kikao kazi cha Washauri wa Mifugo

Jan, 17 2022

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango leo tarehe 17 Januari 2022 amefungua kikao kazi cha Washauri wa Mifugo wa Mikoa na wakuu wa idara za Mifugo na Uvuvi kutoka Mamlaka za Serikali za Mitaa (Tamisemi) kinachofanyika Ukumbi wa Kambarage Jengo la Hazina mkoani Dodoma.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho Makamu wa Rais amesema serikali itaendelea kuipa umuhimu Sekta ya Mifugo hapa nchini kutokana na mchango mkubwa wa sekta hiyo katika kuwainua wananchi kutoka katika lindi la umaskini kwa kutoa ajira na fursa mbalimbali. Amesema sekta hiyo huchangia usalama wa chakula, na upatikanaji wa lishe bora pamoja na malighafi katika viwanda vya kuchakata na kusindika mazao ya mifugo hususani viwanda vya nyama, ngozi na maziwa.

Makamu wa Rais ameagiza kusimamiwa kwa Maafisa Ugani ili kutenda kazi zao kwa ufanisi unaotakiwa. Ameagiza kila Afisa Ugani kuwa na orodha ya wafugaji anaowahudumia, ratiba ya kuwatembelea wafugaji ili kuwashauri na kufuatilia maendeleo ya mifugo, na kupima matokeo ya huduma anazotoa. Makamu wa Rais amesema licha ya Tanzania kuwa nchi ya pili kwa idadi ya mifugo Barani Afrika lakini bado tija ya sekta hiyo hairidhishi kutokana na kukosekana kwa huduma bora za ugani pamoja na wananchi kuendeleza utamaduni wa ufugaji wa kienyeji ambao hauzingatii ubora bali idadi kubwa ya mifugo, hali inayopelekea uwezo mdogo wa kukabiliana na magonjwa ya mifugo, upungufu wa malisho na uharibufu mkubwa wa mazingira na vyanzo vya maji.

Aidha kutokana na athari za mabadiliko ya tabia ya nchi, Makamu wa Rais amewataka watendaji wa Serikali katika ngazi zote kutoa elimu na kusimamia ufugaji kwa utaratibu wa kuingiza mifugo katika maeneo yenye malisho ili kupunguza migogoro ya ardhi pamoja na uharibifu wa mazingira.

Makamu wa Rais amewataka viongozi wa Wizara pamoja na Wakuu wa Idara za Mifugo kuzuia uuzaji wa chanjo na madawa yaliyoisha muda wake pamoja na kuhakikisha chanjo sahihi na madawa ya mifugo vinapatikana katika vijiji na maeneo ya wafugaji. Aidha amewataka kuhakikisha wanapanga matumizi ya ardhi kwa ajili ya mifugo na kilimo cha mazao.

Katika hatua nyingine Makamu wa Rais amekabidhi pikipiki 300 kwa wakuu wa Mikoa wakiwakilishwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Anthony Mtaka ili kutumika kwa kazi za maafisa Ugani katika Halmashauri 140 hapa nchini. Makamu wa Rais ameagiza pikipiki hizo kutumika kwa malengo yaliokusudiwa ambayo ni kuwahudumia wafugaji katika maeneo yao na si vinginevyo.

Kwa upande wake Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mheshimiwa Mashimba Ndaki amesema amesema kikao kazi hicho kinalenga kupata namna bora itayosaidia kuongeza tija, kipato na kuongeza ajira katika sekta ya mifugo nchini. Aidha amesema kutokana na hali ya ukame hapa nchini tayari baadhi ya maeneo yamekabiliwa na upungufu wa malisho ya mifugo na hivyo kupelekea kufa kwa mifugo ambapo Jumla ya Ng’ombe 69751, mbuzi 11024, kondoo 15742 na Punda 1680 zimekufa. Katika kukabiliana na hali hiyo Waziri Ndaki amesema tayari wamezungumza na mamlaka za mabonde ya maji ili kuruhurusu mifugo kupata maji katika maeneo ya mabonde hayo pamoja na kufanya mazungumzo na mamlaka za hifadhi mbalimbali kuruhusu mifugo kupata malisho ndani ya hifadhi ili kunusuru hali hiyo.

Settings