Makamu wa Rais atembelea eneo litalojengwa jengo la Ubalozi wa Tanzania, Kenya

Mar, 04 2022

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango leo tarehe 4 Machi 2022 akiwa Nairobi nchini Kenya ametembelea eneo la Upper Hill ambapo kuna kiwanja cha serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kinachotarajiwa kujengwa jengo la Ghorofa 23 la Ubalozi na kitega uchumi cha Ubalozi.

Akizungumza mara baada ya kukagua eneo hilo, Makamu wa Rais ameagiza Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kuhakikisha ujenzi huo unaanza mara moja kama ilivyopangwa. Amesema tayari serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan imetoa fedha za ujenzi hivyo mkandarasi anapaswa kuendana na kasi ya ujenzi lakini kwa kuzingatia ubora.

Amesema uwepo wa jengo hilo utawezesha Ubalozi wa Tanzania nchini Kenya kujiendesha pamoja na kutumika kuendesha balozi zingine katika maeneo mbalimbali kwa kutumia kitega uchumi hicho.

Ujenzi wa jengo hilo unatarajiwa kuanza mwezi Mei mwaka 2022 na kukamilika baada ya miaka mitatu. Jengo hilo linatarajiwa kutumika katika kupangisha kwaajili ya ofisi na kwa Matumizi ya Ubalozi.

Ubalozi wa Tanzania nchini Kenya wamemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia na kutenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo na kuahidi kushirikiana vema na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kusimamia utekelezaji wa mradi huo muhimu kwa taifa.

Settings