Dkt. Komba: Tanzania iungwe mkono kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi

May, 12 2022

Mkurugenzi wa Mazingira Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Andrew Komba amesema Serikali ya Tanzania inahitaji kuungwa mkono katika jitihada za kukabiliana na athari za mabdiliko ya tabianchi.

Ametoa wito huo leo Mei 12, 2022 wakati wa kikao kati ya wataalamu wa mazingira wa Ofisi ya Makamu wa Rais na washirika wa maendeleo kutoka Ubalozi wa Norway pamoja Shirika la Maendeleo la Norway (NORAD).

Dkt. Komba alitoa wito kwa Serikali ya Norway kuwekeza katika kuongezea nguvu Tanzania katika jitihada za kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi kwa kujenga uwezo wa nchi kitaalamu, rasilimali fedha na teknolojia.

Pia alisisitiza kujengea uwezo Mamlaka za Serikali za Mitaa katika kusimamia sekta ya mazingira ngazi za Mikoa na Wilaya ili kukabiliana na changamoto za kimazingira hasa mabadiliko ya tabianchi ambayo yanaonekana wazi.

Kwa upande wake Mwakilishi kutoka NORAD Bw. Ivar Jamensen alisema Norway iko tayari kutoa ushirikiano katika kuisaidia Tanzania kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Alisema pia watatoa ushirikiano katika kufikia malengo katika utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Mazingira ya mwaka 2021, Mkakati wa Taifa wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi 2021 na Mchango wa Taifa wa Kukabiliana na Mabadilko ya tabianchi (NDC) 2021.

Settings