Dkt. Jafo asitisha uchimbaji usiokidhi sheria ya mazingira

Dec, 31 2021

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Dkt. Selemani Jafo amesitisha shughuli za uchimbaji wa madini ya nickel katika eneo la mlima wa Yobo wilayani Chamwino mkoani Dodoma kutokana na kutokidhi Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004.

Ametoa maelekezo hay oleo Desemba 30, 2021 wakati akiwa katika ziara ya kikazi ya kutembelea na kukagua shughuli za mazingira katika maeneo ya wachimbaji wilayani humo

Dkt. Jafo alimtaka mwekezaji huyo wa kuusajili mradi huo katika ofisi za Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Kanda ya Kati ili wataalamu wajiridhishe kuhusu athari za mazingira katika eneo hilo.

“Hawa watu huko chini wataathrika na athari zinazoweza kutokea kutokana na uchimbaji huu usiofuata matakwa ya sheria na baadaye watakuja kuilaumu Serikali kwa hiyo namuagiza aanze mara moja mchakato wa kupata Cheti cha Athari kwa Mazingira (EIA),” alisema Dkt. Jafo.

Alisema pamoja na kwamba wachimbaji wengi wanadai wana mpango kazi wa kulinda mazingira lakini hauwezi kukidhi matakwa ya Sheria ya Usimamizi wa Mazingira yam waka 2004 hivyo wanawajibika kupata EIA.

Aidha, Waziri Dkt. Jafo alisisitiza kuwa ni kweli tunajenga uchumi hususan katika sekta ya uchimbaji wa madini mbalimbali nchini lakini ni lazima uendane na uhifadhi wa mazingira.

Katika hatua nyingine Waziri huyo akiwa wilayani humo alifanya ziara katika eneo linalochimbwa madini aina ya graphite lililopo Kijiji cha Itiso na kubaini uchimbaji wa mashimo usiofuata taratibu.

Kautokana na hali hiyo alitoa miezi sita kwa Kampuni ya China Dragon inayofanya shughuli hizo hapo kuhakikisha wanakarabati eneo hilo ikiwemo kufukia mashimo hayo ili kukidhi matakwa ya mazingira.

Pia alitoa mwezi mmoja kwa kampuni kuja na mpango kazi wa namna gani watatekeleza maelezo hayo huku akiiagiza NEMC Kanda ya Kati kumpa taarifa ya utekelezaji wa agizo ndani ya kipindi hicho.

Settings