Zungu: Serikali yatekeleza miradi kuondosha hewa ya ukaa

Mar, 21 2020

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mussa Azzan Zungu amesema miradi ya reli ya kisasa (SGR), mradi wa kufua umeme wa Mto Rufiji na mabasi ya mwendo kasi (DART) ni jitihada za Serikali katika kupambana na athari za hewa ya ukaa.

Zungu alisema hayo leo wakati alipotembelea Kituo cha Taifa cha Ufuatiliaji Hewa ya Ukaa (NCMC) kilichopo katika Chuo cha Kilimo (SUA) mjini Morogoro ambapo alikipongeza na kuahidi kuzifanyia kazi changamoto zake.

Alisema pamoja na jitihada hizo za Serikali za kupambana na hewa ya ukaa lakini pia alitoa rai kwa wananchi kutumia nishati mbadala, kupanda miti ambayo kwa namna moja inasaidia katika kupunguza hewa ya ukaa.

Akifafanua zaidi waziri huyo alitahdharisha kuwa hewa ya ukaa inaeweza kuwa na athari kubwa kwa vizazi vijavyo kama hatutaamua kuchukua hatua katika kupambana na changamoto hiyo.

Alipongeza jitihada zinazofanywa na Serikali lakini pia alitoa mwito kwa wananchi ambao ni wadau wakubwa wa mazingira ili watoe mchango wao na kushirikiana na Serikali katika kuondokana changamoto hiyo.

“Tunataka sasa wananchi wajue madhara ya kulima kwenye vyanzo vya maji na athari ya hewa ukaa inatokana na shughuli za kibinadamu hasa ukataji wa miti na tumesikia taarifa hapa ya namna miti inavyopotea kuanzia mwaka 2002 hadi mwaka 2013 miti takriban 464,000 imepotea hii ni hatari kwani inaweza kusababisha nchi kuelekea kuwa jangwa,” alisema.

Akipingeza NCMC kwa kazi nzuri wanayofanya waziri huyo aliwaomba wakamilishe taratibu ili waweze kupata fedha kutoka Hazina ambazo zitasaidia kukifanya kituo kiwe chini hya SUA badala ya kutegemea wafadhili kutoka nje.

Awali akiwasilisha mada Mratibu wa kituo hicho, Profesa Eliakimu Zabibu alisema Tanzania ambayo ni nchi mwanachama wa Mkataba wa

Umoja wa Mataifa Mabadiliko ya Tabianchi (UNFCCC) inaweza kufaidika na sera kama Mpango wa Kupunguza Uzalishaji wa Hewa Ukaa kutokana na ukataji miti ovyo na uharibifu wa Misitu’ – MKUHUMI (REDD+).

Profesa Zabibu alisema faida za MKUHUMI ni kuimarisha utunzaji misitu nchini,kupata fedha kutoka vyanzo mbalimbali.

Ili nchi iweze kushiriki katika shughuli za MKUHUMI ni sharti ikamilishe vigezo vya kuandaa Mkakati wa Kitaifa wa Upunguzaji wa Hewa Ukaa pamoja na Mpango kazi, kuandaa Takwimu za Msingi za Kiwango Rejea cha Hewa

Ukaa kinachozalishwa kutokana na upotevu na uharibifu wa misitu nchini (Forest Reference Emission Level- FREL); Kuanzisha mfumo madhubuti wa Upimaji, Uwasilishaji na Uhakiki wa Kaboni (Measurement, Reporting and Verification- MRV System);

Kuweka mfumo wa Kinga za Athari zinazoweza kutokea kutokana na utekelezaji wa shughuli za MKUHUMI (REDD+Safeguard System); na Kuandaa mfumo wa Wazi na Thabiti wa Malipo yatokanayo na utekelezaji wa MKUHUMI.

Settings