​Waziri Ummy awasilisha taarifa ya miradi ya Ofisi ya Makamu wa Rais kwa Kamati ya Bunge

Mar, 10 2021

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Ummy Mwalimu amewasilisha taarifa ya utekelezaji wa miradi mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira katika Ofisi za Bunge jijini Dodoma leo.

Akizungumza mara baada ya kuwasilisha taarifa hiyo alisema Serikali itasambaza Mwongozo wa usafishaji mito kwa kuondoa mchanga, tope na taka ngumu Mkoa wa Dar es Salaam kwa wadau wote.

Katika kikao hicho miongoni mwa taarifa za miradi zilizowasilishwa ni Mradi wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi kwa kutumia Mifumo Ikolojia Vijijini (Ecosystem-Based Adaptation for Rural Resilience in Tanzania (EBARR).

Taarifa nyingine ni ya Mradi wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi katika eneo la Unguja – Zanzibar na muhtasari wa hali ya usimamiziwa mazingira katika mto nyakasangwa na mito mingine.

Itakumbukwa Februari 8, 2021 Waziri Ummy alifanya mkutano na wachimbaji mchanga katika Mkoa wa Dar es Salaam kwa lengo la kusikiliza changamoto wanazokabiliana nazo hususan masuala ya vibali vya kusafisha mito na mabonde.

Katika kuhitimisha mkutano alielekeza kuwa Katibu Tawala wa Mkoa huo kwa kushirikiana na Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Higffadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) waitishe kikao cha Kikosi Kazi ili kuandaa Mwongozo wa Usafishaji Mito na Mabonde kwa Mkoa wa Dar es Salaam na Pwani.

Hivyo kutokana na maelekezo hayo Februari 12, 2021 Katibu Tawala akishirikiana na Mkurugenzi Mkuu wa NEMC waliitisha kikao cha Kikosi Kazi na kuandaa Mwongozo wa Usafishaji Mito na Mabonde mkoa huo.

Settings