Kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira, Sura ya 191 na Kanuni zake, Ofisi ya Makamu wa Rais imepewa Mamlaka ya kusimamia na kuratibu masuala yote yanayohusu Mazingira nchini. Kifungu cha 133(1) na (3) cha Sheria ya Usimamizi wa Mazingira Sura ya 191 pamoja na Kanuni za Usimamizi na Udhibiti wa Taka Hatarishi za Mwaka 2021, zinampa Mamlaka Waziri mwenye dhamana ya Mazingira kutoa vibali vya kukusanya, kuhifadhi, kusafirisha ndani ya nchi, kuingiza nchini, kusafirisha nje ya nchi na kupitisha nchini taka hatarishi.
Aidha, taka hatarishi au taka zenye madhara ni pamoja na vyuma chakavu, taka za kieletroniki, dutu hatarishi, mafuta machafu, matairi chakavu, taka za plastiki, taka zitokanazo na huduma za kitabibu, betri zilizotumika na aina ya taka zote zinazotoka migodini.
Taka hizi hatarishi zinaweza kusabisha athari kwa afya ya binadamu, viumbe hai na mazingira. Ili kuzuia na kudhibiti athari hizo zitokanazo na taka zenye madhara, mfumo mahsusi unaofanya kazi kwa ufanisi wa kudhibiti taka hizi unapaswa ufuatwe kama ulivyobainishwa kwenye Sheria ya Usimamizi wa Mazingira Sura ya 191 na Kanuni zake.