Waitara avitaka viwanda viwe na wataalamu wa mazingira kukidhi matakwa ya sheria

Mar, 15 2021

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mwita Waitara amewaagiza wenye viwanda wote nchini kuajiri wataalamu wa mazingira ili kukidhi matakwa ya kisheria.

Waitara ametoa maagizo hayo alipofanya ziara ya kikazi ya kutembelea viwanda mbalimbali vilivyopo maeneo ya Mlandizi na Kibaha wilayani Kibaha mkoani Pwani kwa lengo la kukagua uzingatia wa Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004.

Aidha ameliagiza Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kufanya ukaguzi wa mazingira katika viwanda vilivyopo wilayani humo ili kuona kama wanatunza mazingira kisha kuandaa ripoti itakayoisaidia Serikali kutoa maamuzi ili kuwalinda wananchi na uchafuzi wa mazingira.

Pamoja na kuwapongeza wawekezaji wa viwanda aliwataka kufuata sheria na kusisitiza kuwa Serikali haitafungia kiwanda chochote na badala yake itawasaidia kukidhi matakwa ya sheria.

Hata hivyo kutokana na hali aliyoikuta alipotembelea na kukagua kiwanda cha Keds Tanzania Company Ltd alikutana na utiririshaji wa majitaka bila kuyatibu jambo linaloweza kusababisha athari kwa mazingira na wananchi ambapo alisema ni kosa kisheria.

Kutokanana hali hiyo Waitara alitoa siku 14 kwa kiwanda hicho kuyafanyia kazi maagizo waliyopewa na NEMC na kuhakikisha wanaacha mara moja kutiririsha maji hao sambamba na kuwa na mtambo wa kuchakata taka ambazo wanazalisha ili kuepusha kusambaa hovyo kwa taka.

“Wawekezaji tunawapenda ili ni lazima mfuate sheria kwa mfano kiwanda kimoja tumebaini mtu hana hata cheti za Tathmini ya Athari kwa Mazingira, amechimba tu bwawa la kutibu majitaka bila kufuata utaalamu na maji yanakwenda chini hatujui yana sumu kiasi gani, wananchi wanachimba kisima wanachimnba kisima anapata sumu, kwa hiyo NEMC mje hapa mfanye ukaguzi,” alisema.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Utekelezaji na Uzingatiaji wa Sheria (NEMC) Edgar Mgila alibainisha kuwa kiwanda hicho kinatumia makaa ya mawe kama chanzo cha nishati jambo ambalo ni zuri katika njia ya utunzaji wa mazingira, lakini shida iliyopo ni namna ya kuhifadhi makaa hayo.

Mgila alifafanua kumekuwa na malalamiko mengi kutoka kwa wakazi wa maeneo ya jirani kuhusu ya majitaka kutoka kiwandani na kuharibu mazingira hivyo Baraza hilo lilimuelekeza mwekezaji huyo namna ya kuhifadhi makaa hayo na kutoa muda wa kuhakikisha hawatiririshi maji kwenda kwenye mazingira.

Katika ziara hiyo pia Naibu Waziri Waitara akiwa ameambatana na watendaji kutoka NEMC na Wilaya ya Kibaha alitembelea viwanda vya Sunda Chemical Fibres, Fuxing Ltd na Kiluwa Steels Group Company Limited.

Settings