Ofisi Ya Makamu Wa Rais, Iucn Wakutana Na Kamati Za Maliasili Na Mazingira Za Vijiji 31 Kujadili Mradi Slr

Dec, 06 2023

Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Uhifadhi wa Mazingira (IUCN) imeendesha mafunzo kwa kamati za maliasili na mazingira za vijiji 31 kutoka Kata 10 zilizopo katika Bonde la Mto Ruaha Mkuu vinavyotekeleza Mradi wa Urejeshwaji Endelevu wa Mazingira na Hifadhi ya Bioanuai (SLR).

Akifungua mafunzo hayo leo Desemba 6, 2023 Jijijini Mbeya, Mratibu wa Kitaifa wa Mradi wa SLR, Dkt. Damas Mapunda amesema mafunzo hayo ya awamu ya kwanza ni sehemu ya Utekelezaji Mpango Mkakati wa Mradi huo yametolewa kwa kamati za vijiji za Halmashauri nne za Wangingo’ombe (Njombe), Mbarali Mbeya, Mbeya Vijijini (Mbeya) na Vijijini Iringa (Iringa).

Dkt. Mapunda amesema malengo ya mafunzo hayo ni kuzijengea uwezo kamati za maliasili na mazingira za vijiji katika uandaaji wa mipango ya matumizi bora ya ardhi sambamba na urejeshaji uoto wa asili ili kuwa na uzalishaji wenye tija wa mazao ya kilimo na mifugo.

“Madhara ya uharibifu wa uoto wa asili ikiwemo ukataji wa miti sambamba na mabadiliko ya tabianchi yameonekana wazi katika maeneo mengi ya nchi na yamegusa maeneo mengi ya uchumi wa nchi, hivyo tumekutana kama wadau ili kuwa mjadala wenye tija kwa ajili ya kusaidia maeneo yetu” amesema Dkt. Mapunda.

Dkt. Mapunda kamati za maliasili na mazingira za vijiji ambazo zimeanzishwa chini ya Sheria ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa ya mwaka 1987 ni nguzo muhimu katika urejeshaji wa uoto wa asili na hifadhi za bianuai kwani kamati hizo ndizo zilizopewa mamlaka ya kusimamia masuala ya maliasili na mazingira katika maeneo ya vijiji vyote nchini.

Ameongeza kuwa kutokana na umuhimu wa kamati katika mradi, Ofisi ya Makamu wa Rais na IUCN imetoa mafunzo hayo ili kuziwezesha kamati hizo kuelewa dhamira na dhana ya mradi huo katika maeneo yao na hatimaye kuleta matokeo chanya katika jamii zinazozunguka mradi.

Aidha ameongeza kuwa mbali na kuhifadhi mazingira yaliyoharibika, mradi wa SLR pia umelenga kuhakikisha kuwajamii zinazoishi maeneo yenye uoto wa asili zinaweza kujiinua kiuchumi na kuimarisha uwezo wa wananchi kushiriki katika shughuli rafiki za utunzaji wa uhifadhi wa misitu kupitia kamati za mazingira zilizoundwa na vijiji husika.

Kwa mujibu wa Dkt. Mapunda amesema katika msimu wa kilimo uliopita, Mradi uliweza kuanzisha jumla ya mashamba darasa 30 katika vijiji vilivyopo katika Bonde la Ruaha Mkuu vinavyotekeleza mradi ambapo wakulima na wafugali walipatiwa mafunzo na mbinu mbalimbali za uendeshaji shughuli za kilimo na ufugaji ambazo ni rafiki kwa mazingira.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mapunda amesema mradi huo kwa kushirikiana na Tume ya Taifa Mipango ya Matumizi ya Ardhi (NLUPC) imepanga kupima jumla ya vijiji 42 sambamba na kutoa hati miliki za kimila zipatazo 4500 katika vijiji vilivyopo ndani ya mradi wa SLR unaotekelezwa katika Mikoa mitano na Halmashauri saba nchini.

Kwa upande wake, Mshauri wa Ufundi kutoka IUCN, Bw. Doyi Mazenzele amesema Shirika hilo kwa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais imekuwa ikitoa mafunzo ya kitaalamu na kiufundi kwa watendaji na viongozi wa ngazi ya Kijiji, kata na Halmashauri na taasisi za kitaifa zinazosimamia mradi huo.

“Tumeanza kutoa mafunzo haya kwa kamati za maliasili na mazingira za vijiji kwa ajili ya kuwajengea uwezo na kamati zinazojihusisha na usimamizi wa rasilimali za maji, jumuiya za watumiaji maji na hatua inayofuata tutakwenda kwa wakulima, wafugaji pamoja na Asazi Zisizo za Serikali (AZISE) zilizopo ngazi ya vijiji” amesema Mazenzele.

Naye mshiriki wa mafunzo hayo, Bi. Leticia Badengeya ambaye ni Mjumbe wa Kamati ya Maliasili na Mazingira kutoka Kijiji Uwengu Halmashauri ya Wilaya ya Wanging’ombe Mkoani Njombe ameishukuru Ofisi ya Makamu wa Rais na IUCN kwa kuandaa mafunzo hayo kwani mradi wa SLR umeleta matokeo chanya katika Kijiji hicho ikiwemo utunzaji wa vyanzo vya maji.

Mradi wa SLR unafadhiliwa na Mfuko wa Mazingira wa Dunia (GEF) kupitia Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP) na kusimamiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais ambapo kiasi cha Bilioni 25.8 kimetengwa kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo.

Mradi huo wa miaka mitano ulioanza mwaka 2021 unatarajia kukamilika mwaka 2025 ambapo jumla ya Mikoa 5, Halmashauri 7, Kata 18 na vijiji 54 vinatarajia kunufaika na mradi huo. Halmashauri zinazonufaika na mradi ni Iringa Vijijini (Iringa), Wilaya ya Mbeya na Mbarali (Mbeya), Halmashauri za Sumbawanga vijijini (Rukwa) pamoja na Halmashauri za Wilaya za Tanganyika na Mpimbwe (Katavi).

Settings