DUWASA yatakiwa kupata cheti cha mazingira kujenga mabwawa ya majitaka

Apr, 29 2021

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Selemani Jafo ameipa wiki moja Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mjini Dodoma (DUWASA) kuomba Cheti cha Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM) katika mradi wa ujenzi wa mabwawa ya majitaka yanayotarajiwa kujengwa katika katika eneo la Nzuguni jijini humo.

Jafo ametoa maelekezo hayo leo Aprili 29, 2021 alipofanya ziara ya kushtukiza katika mabwawa katika maeneo ya Hospitali ya Benjamin Mkapa na Swaswa jijini humo kukagua udhibiti wa majitaka.

Alisema kabla ya kuanza kujenga mradi wowote ni lazima kuanza mchakato wa kupata cheti cha TAM ambacho kinatoa mwongozo wa namna hya kujenga mradi huo.

“Mkurugenzi haya mabwawa ni sensitive sana kwa maisha ya watu sasa nitoe maelekezo muwasiliane na NEMC (Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira) tena wako hapa Dodoma anzeni mchakato wa kupata cheti na mtoe ushauri mbainishe changamoto na njia za kutatua kuhusu ujenzi huu,” alisema Jafo.

“Alhamisi ijayo niwaone tayari mmeanza mchakato na uzuri kila kitu kipo kwenye mfumo na nimetoa maelekezo, utaratibu wa kupata cheti usichelewe na ndiyo maana zaidi ya maombi 862 ya vyeti yamekuja na vyeti 30 vingine tayari vimeshatolewa,” aliongeza.

Pia aliitaka DUWASA kuanza mara moja ujenzi wa mabwawa katika eneo jipya la Nzuguni kwa kuwa eneo la Swaswa yalipo mabwawa hayo ni eneo la makazi na hivyo kuleta kero kwa wananchi wanaozunguka.

Hata hivyo alimpongeza Mkurugenzi wa DUWASA Mhandisi Aron Joseph kwa kuwa na mikakati mizuri katika usimamizi wa majitaka na kumuahidi kuzungumza na mawaziri wenye dhamana ya Fedha na Mipango pamoja na Maji ili kuwezesha upatikanaji wa rasilimali fedha kwa haraka ili ujenzi uanze haraka iwezekanavyo.

Aidha waziri huyo alionesha kutoridhishwa na udhibiti wa majitaka katika mabwawa yaliyopo Hospitali ya Benjamin Mkapa ambapo pia alitoa wiki moja kwa uongozi wa DUWASA kuboresha eneo hilo ili kulinda afya za wananchi.

“Sijaridhika na hali nayoioana hapa huu uchafu unaovuja katika chemba hii kama mvua kubwa ikinyesha unaeweza kutiririka kwenye vyanzo vya maji na kuleta athari za kiafya kwa wananchi, name siwezi kuvumilia kuna wananchi wanaathirika sasa wiki moja hapa patengenezwe,” alisema Jafo.

Settings