Waziri Jafo, Balozi wa Norway wajadili ushirikiano katika nishati safi

Nov, 21 2023

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Norway nchini Tanzania Mhe. Tine Tonnes.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika Ofisi ndogo ya Makamu wa Rais jijini Dar es Salaam Novemba 21, 2023 viongozi hao wamejadili kuhusu utekelezaji wa miradi ya nishati safi ya kupikia.

Dkt. Jafo amemueleza Balozi Tinnes dhamira ya Serikali katika kuimarisha upatikanaji wa nishati safi na kuachana na matumizi ya kuni na mkaa kwa kuanza na taasisi zenye kulisha idadi kubwa ya watu.

Amesema Serikali inaendelea kuwekeza na kuhimiza matumizi ya nishati safi ya kupikia hususan ya gesi katika shule na vyuo mbalimbali ili ziachane na matumizi ya kuni na mkaa ambayo inaonekana kuwa ni ya gharama zaidi.

Amesema Serikali inaendelea kuimarisha mradi wa nishati ya gesi kusini mwa Tanzania ambao utakuwa chachu katika hifadhi ya mazingira kwa kupunguza ukataji miti.

Aidha, Waziri Jafo ameishukuru Serikali ya Norway kwa kuiunga mkono Tanzania katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi zikiwemo utoaji wa fedha zaidi ya shilingi 16 hivi karibuni.

"Tunaishukuru sana Norway kwa kuwa nasi bega kwa bega katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na tunaweza kukumbuka tulisaini makubaliano ambayo yalitupatia zaidi ya shilingi bilioni 7 na ule mradi wa utafiti COSTECH bilioni 9 hayo yote ni matunda ya uhusiano baina yetu," amesema Dkt. Jafo.

Kwa upande wake Balozi Tinnes amesema kuwa dhamira ya Serikali yake ni kuwekeza katika miradi ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi hasa katika nishati safi.

Baadhi ya miradi ambayo Balozi ameitaja ni pamoja na uwekezaji atika nishati ya baiogesi, umeme unaozalishwa na maji pamoja na usimamizi wa taka ngumu.

Ameelezea dhamira ya kampuni mbalimbali kutoka Norway kuwekeza katika gesi ambayo itasaidi kupunguza vitendo vya ukataji wa miti kwa ajili ya nishati ya kupikia.

Settings