Waziri Jafo awasilisha Bajeti ya mwaka 2024/25

Apr, 23 2024

Ofisi ya Makamu wa Rais inaandaa Mfumo wa Kieletroniki wa Uratibu wa Taarifa za Masuala ya Muungano na yasiyo ya Muungano.

Pia, inaanzisha Kituo cha Kumbukumbu na Nyaraka za Muungano wa Tanganyika na Zanzibar (MAKAVAZI) ili kuwa na mfumo endelevu wa kuhifadhi kumbukumbu na nyaraka za mambo ya Muungano ili kuongeza uelewa wa masuala ya Muungano kwa kizazi cha sasa na kijacho.

Hayo yamebainishwa bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo wakati akiwasilisha Bajeti ya mwaka wa fedha 2024/25 leo Aprili 23, 2024.

Akizungumzia mfumo huo amesema lengo ni kurahisisha, upatikanaji, uandaaji, uchambuzi na uunganishaji wa taarifa za utekelezaji wa masuala ya Muungano na yasiyo ya Muungano.

Ili kujenga uelewa wa pamoja kuhusu utekelezaji wa masuala ya Muungano na yasiyo ya Muungano, Dkt. Jafo amesema Ofisi ya Makamu wa Rais itatoa mafunzo kwa Maafisa Viungo wa Wizara na Taasisi za Muungano.

Aidha, katika kuzitafutia ufumbuzi hoja nne za Muungano zilizopo, Ofisi itaratibu vikao vya Kamati ya Pamoja ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SJMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) katika ngazi ya Makatibu Wakuu, Mawaziri na Kamati ya Pamoja.

“Kutakuwa na Vikao vya Kamati Ndogo za Fedha, Uchumi na Biashara, Kamati ya Sheria, Katiba na Utawala vitakavyofanyika kulingana na mahitaji lengo likiwa ni kutatua hoja hizo nne zilizobakia,” amefafanua.

Kwa upande wa mazingira, Waziri Jafo amesema Ofisi imeandaa Mradi wa Kuhimili Athari za Mafuriko na Kuongeza Usalama wa Chakula Katika Maeneo yanayoathiriwa na Mafuriko Nchini.

Amesema lengo la mradi huu ni kuijengea uwezo jamii katika kuhimili athari za mafuriko kwa kuwa na shughuli endelevu za kujipatia kipato na kuongeza usalama wa chakula katika maeneo yaliyoathirika.

“Katika mwaka 2024/25 kiasi cha shilingi bilioni 1.1 kimetengwa kwa ajili ya kufanya upembuzi katika maeneo yaliyoathirika na mafuriko katika Jiji la Dar es Salaam, kufanya usanifu wa kina wa miundombinu inayopendekezwa katika maeneo yaliyoathirika na mafuriko na Kuanza ujenzi katika baadhi ya maeneo yatakayopendekezwa,” amefafanua.

Katika hatua nyingine ametaja vipaumbele vitakavyotekelezwa kwa mwaka 2024/25 vikiwemo kuratibu utekelezaji wa Sera na Sheria ya Usimamizi wa Mazingira Sura 191.

Amesema kuwa pia, Ofisi ya Ofisi ya Makamu wa Rais itaendelea simamia utekelezaji wa Mpango Kabambe wa Taifa wa Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira 2022-2032 kwa kuhamasisha matumizi na uwekezaji wa teknolojia za nishati safi ya kupikia, kuratibu na kufuatilia utekelezaji wa agizo la Serikali kwa taasisi za umma zenye watu zaidi ya 100 kutumia nishati safi.

Halikadhalika, katika kudumisha Muungano, Dkt. Jafo amesema Ofisi itaendelea kuratibu na kuendesha vikao vya ushirikiano na SMZ katika masuala ya hifadhi na usimamizi wa Mazingira.

Hivyo, Waziri Dkt. Jafo ameliomba Bunge liidhinishe jumla ya shilingi 62,686,762,000 kwa ajili ya Ofisi ya Makamu wa Rais katika kipindi cha mwaka wa fedha 2024/25.

Settings