Waziri Jafo ahimiza weledi kwa washauri elekezi wa mazingira

Nov, 21 2023

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo amewataka washauri elekezi wa mazingira kufanya kazi kwa weledi na maadili ili kufikia malengo ya utekelezaji wa miradi.

Ametoa wito huo wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Tano wa mwaka wa Chama cha Washauri Elekezi wa Mazingira Tanzania (TEEA) leo Novemba 21, 2023 jijini Dar es Salaam.

Dkt. Jafo amesema wataalamu wa mazingira ni wadau muhimu katika ajenda ya uwekezaji ambao unategemea Cheti cha Tathmni ya Athari kwa Mazingira (TAM) hivyo wanapaswa kufanya kazi kwa ufanisi.

Amesema uwekezaji wowote unahitaji andiko la cheti ambacho ni mwongozo wa uwekezaji hivyo lazima uzingatie takwimu hasa katika masuala ya hali ya hewa ili kutoa cheti kinachozingatia matakwa ya hali ya hewa kwa mfano ujenzi wa madaraja unaozingatia ustahimilivu wa mvua.

“Naombeni niwaambie ndugu zangu, leo hii inawezekana kuna baadhi ya watu hawajui thamani yenu ninyi wataalamu wa mazingira tunashuhudia katika kipindi cha miaka mitatu, miradi 7,195 imetekelezwa kwa sababu mmeifanyia tathmini,” amesema Dkt. Jafo.

Ameongeza kuwa miradi yote yenye kuhitaji uwekezaji wa mashirika makubwa ya fedha duniani hauwezi kupata fedha bila kuwa imefanyiwa ukaguzi na kupata vyeti vya TAM.

Aidha Mhe. Jafo amewataka wataalamu hao kutoa ushauri wa mazingira kwa wawekezaji ili kuwepo na uwekezaji wenye tija na manufaa katika jamii huku akisema mfumo wa kusajili miradi umekuwa na mafanikio.

Hali kadhalika Waziri Jafo ametoa wito kwa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuwajengea uwezo wataalamu wa mazingira ili wapate maarifa Zaidi ya utekelezaji wa tathmni ya athari kwa mazingira na kupitisha miradi.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa TEEA Bw. Emmanuel Hanai Amesema wataamu elekezi hao wakitumiwa vizuri watakuwa mfano mzuri katika kuelimisha jamii kulinda mazingira.

Mwakilishi wa Mkurugenzi wa NEMC Bi. Lilian Lukambuzi amesema Baraza hilo litaedneela kushirikiana na wadau wa mazingira wakiwemo wataalamu elekezi ili kuhifadhi mazingira.

Amesema litaendelea kuwapokea na kuwasikiliza washauri elekezi kwa lengo la kujadili changamoto mbalimbali zinazowakabili hususan katika utekelezaji wa majukumu zikiwemo kanuni.

Bi. Lilian ameongeza kuwa Baraza hilo tayari limefanikiwa kusajili jumla ya wataalamu elekezi 1,764 ambao kati yao 1,056 ni wa binafsi.

Settings