Viongozi wa dini watakiwa kutoa mafundisho ulinzi wa mazingira

May, 02 2024

Serikali imetoa wito kwa viongozi wa dini kuendelea kutoa mafundisho kwa waumini na jamii kwa ujumla kuhusu kulinda rasilimali za dunia kwa ustawi wa viumbe vyote na mazingira.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis wakati akizindua Jukwaa la Uwakili linaloundwa na viongozi wa dini wa Kanda ya Ziwa ambao kupitia wanashiriki katika utunzaji wa mazingira, uzinduzi uliofanyika mkoani Mwanza leo tarehe 02, 2024.

Mhe. Khamis amesema Jukwaa hilo lina jukumu la kuongoza kuelekea malengo ya utunzajii wa mazingira. Amesema kuwa Jukwaa la Uwakili ni mfano mzuri wa kuunganisha nguvu kwa pamoja katika kuhamasisha jamii kushiriki katika utunzaji wa mazingira kwa maendeleo endelevu.

Amesema mafundisho ya kidini kutoka kwa viongozi hao wa dini yanatukumbusha kuhusu wajibu wetu kama wasimamizi wa dunia, kuhamasisha kuchukua hatua ya kulinda ardhi narasilimali zake muhimu kwa ajili ya ustawi wa viumbe vyote.

Ameongeza kuwa Tanzania inakabiliwa na changamoto za mazingira zikiwemo uharibifu wa ardhi, uharibifu wa vyanzo vya maji, athari za mabadiliko ya tabianchi, uchafuzi wa mazingira, ukataji ovyo wa miti na uharibifu wa misitu ambazo zinahusishwa na changamoto za mfumo wa usimamizi wa mazingira.

“Kufuatana na Sera, Sheria ya Usimaizi wa Mazingira Sura 191, Kanuni na Miongozo inayohusu hifadhi ya mazingira kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Idara ya Mazingira tutajipanga na kupanga mikakati ya kushughulikia changamoto mtambuka zinazohusu usimamizi endelevu wa hifadhi ya mazingira kwa kuhamasisha kuingizwa kwa vipengele vya mazingira katika mifumo ya maendeleo ya sekta nyingine,” amesisitiza Mhe. Khamis.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Said Mtanda amewahimiza wananchi na taasisi mbalimbali zilizopo mkoani humo kuongeza kasi ya upandaji miti ili kukabiliana na athai za mabadiliko ya tabiancgi.

Pia, ametumia nafasi hiyo kutoa wito kwa wananchi kuunga mkono juhudi za Serikali katika jitihada za kuhifadhi mazingira kwa kutumia nishati safi ya kupikia na kuachana na kuni na mkaa yanayochangia kukatwa miti ovyo.

Awali, Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dkt. Alex Malasusa ameipongeza Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais pamoja wadau kutoka mashirika mbalimbali wanaounga mkono juhudi hizo za utunzaji wa mazingira nchini.

Amesema rasilimali zisipotunzwa zitapotea hivyo ushirikano kati ya Kanisa, Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) Mkoa wa Mwanza, Serikali na wadau wengine katika kuhakikisha mazingira yanahifadhiwa ni wa umuhimu.

Hafla hiyo ya Uzinduzi huo umehudhuriwa pia na Mwenyekiti wa BAKWATA Mkoa wa Mwanza Sheikh Moshi Shaban.

Settings