Serikali, wadau yaweka mikakati chupa za plastiki

Apr, 09 2024

Serikali na wadau imeweka mkakati wa kuhakikisha chupa za plastiki za maji na vinywaji hazitupwi ovyo na kuzagaa hali inayochangia uchafuzi wa mazingira.

Hayo yamebainika katika kikao kati ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo na Shirika la PETpro Tanzania linalosimamia urejelezaji wa chupa za plastiki.

Katika mazungumzo na Mratibu Mkazi wa shirika hilo Bw. Nicholaus Ambwene aliyeambatana na Mchambuzi Oliva Gabriel, Dkt. Jafo amesema Serikali inatarajia kuwashirikisha wazalishaji wa chupa za plastiki kuhakikisha urejelezaji unafanyika inavyotakiwa.

Amesema tatizo la kuzagaa kwa chupa za plastiki limekuwa kubwa hivyo ipo haja ya kuwashirikisha wadau wa uzalishaji wa chupa hizo zinazotumuka kuhifadhia maji na vinywaji katika kuhakikisha changamoto hiyo inamalizika.

Dkt. Jafo amelipongeza shirika hilo kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuhakikisha wadau wa uzalishaji wa chupa za plastiki wanashiriki kikamilifu usimamizi endelevu wa chupa hizo.

Awali Mratibu Mkazi wa shirika hilo Bw. Ambwene amewasilisha mrejesho wa shughuli zinazofanywa na PETpro tangu kuanzishwa kwake, maoni, changamoto na mikakakati endelevu.

Pia, amewasilisha namna shirika linavyoshirikiana na Serikali ili kuweka misingi imara ya ushirikishwaji na kuongeza tija katika kuhakikisha usimamizi na wajibu wa wazalishaji baada ya matumizi ya bidhaa zao ili kupunguza athari za kimazingira.

Settings