Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango amewataka Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) kutumia Mitambo ya uchimbaji visima ilionunuliwa na serikali kwa matumizi yaliokusudiwa ikiwemo kutoa huduma kwa wananchi kwa gharama nafuu.
Makamu wa Rais amesema hayo wakati akikagua magari na mitambo ya uchimbaji visima na mabwawa yaliokabidhiwa kwa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) wakati wa hafla ya Uzinduzi wa Taarifa ya Utendaji wa Mamlaka za Majisafi na Usafi wa Mazingira kwa mwaka 2021/2022 iliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es salaam leo tarehe 20 Machi 2023.
Amekemea mitambo hiyo kutumika kwa matumizi binafsi na kuagiza RUWASA kutambua wanapaswa kutoa huduma zaidi kwa wananchi kuliko kufanya biashara. Aidha Makamu wa Rais ameagiza kufanyika tathmini ya bei zinazotumika na RUWASA kuchimba visima binafsi vya wananchi ili kuhakikisha haziwi juu zaidi ya bei za kampuni binafsi.
Halikadhalika Makamu wa Rais amesema serikali inaendelea kutafuta njia bora na fupi zaidi katika utoaji wa msamaha wa kodi ili kuharakisha utekelezaji wa miradi mbalimbali hapa nchini ikiwemo miradi ya maji.
Akihutubia viongozi wa mamlaka za majisafi na usafi wa mazingira hapa nchini, Makamu wa Rais amewataka kuacha kufanya kazi kwa mazoea ikiwemo kuzoea matatizo ya wateja na hivyo kutotimiza majukumu yao kwa ufanisi. Pia Makamu wa Rais amekemea uwepo watumishi ndani ya Mamlaka za Maji ambao si waajiriwa (vishoka) wanaoendelea kuchafua Wizara na Mamlaka za Maji kwani ndio wanawaunganishia maji Wananchi bila kufuata utaratibu na kusababisha malalamiko mengi na baadhi ya maeneo kukosa huduma hiyo.
Aidha Makamu wa Rais ameziasa Mamlaka za Maji kujiwekea mikakati ya kuboresha huduma, kufanya kazi kwa kujituma, uzalendo, uadilifu na kwa weledi ili Mamlaka hizo ziweze kujiendesha kibiashara kwani huduma za usambazaji wa maji zinazotolewa hivi sasa haziendani na mapato yanayokusanywa.