Makamu wa Rais atoa rai kwa walezi kulea watoto kwa kuzingatia maadili

Mar, 23 2023

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip isdor Mpango ametoa wito kwa wazazi na walezi kuwalea watoto kwa kuzingatia maadili ya kitanzania pamoja na kuongeza umakini katika maudhui yanayooneshwa katika televisheni.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati akizungumza na waumini wa Kijiji cha kasumo mkoani Kigoma mara baada ya kushiriki Ibada ya kawaida ya katikati ya wiki katika Kanisa Katoliki Parokia ya Bikira Maria Malkia wa Amani iliopo Kijiji hapo.

Amesema ni wazi kwa sasa kumekuwepo na changamoto ya mmomonyoko wa maadili ikiwemo ndoa za jinsia moja ambapo wazazi, walezi na jamii kwa ujumla inapaswa kukemea vikali ili kuondokana na taifa lisilofaa kwa vizazi vya sasa na baadaye.

Halikadhalika Makamu wa Rais amewaasa wananchi wa Kasumo na Mkoa wa Kigoma kwa ujumla kutoa ushirikiano wakati huu ambapo serikali inafanya ujenzi wa miundombinu ya barabara katika mkoa huo ambayo ni nyenzo muhimu kwa biashara na urahisi wa kufikia huduma za jamii kama vile hospitali na shule.

Aidha amewataka kutoa ushirikiano kwa wawekezaji ikiwemo kuzingatia bei halisi za ardhi katika maeneo yao ili kutowapoteza wawekezaji hao. Makamu wa Rais amewasihi wananchi wa Kasumo kujitolea kwa hali na mali katika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo kijijini hapo ikiwemo ya huduma za afya.

Ibada hiyo iliofanyika leo tarehe 23 Julai 2023 imehudhuriwa na mke wa Makamu wa Rais Mama Mbonimpaye Mpango na kuongozwa na Paroko wa Parokia hiyo Padre Joseph Mashaka.

Settings