Dkt. Mpango: Sekta binafsi zitoe fursa kwa wanafunzi wa vyuo vya ufundi

Feb, 22 2024

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango ametoa wito kwa sekta binafsi nchini kutoa fursa kwa wanafunzi wa vyuo vya ufundi stadi ili waweze kufanya mafunzo kwa vitendo na kuendeleza ujuzi wanaopata katika vyuo.

Makamu wa Rais amesema hayo mara baada ya kuweka Jiwe la Msingi la Chuo Cha Ufundi Stadi (VETA) Wilaya ya Mkinga akiwa ziarani mkoani Tanga. Aidha amewasihi wanafunzi wanaopata elimu chuoni hapo kuzingatia masomo na kujifunza kwa bidii ili ujuzi wanaopata uweze kulinufaisha Taifa.

Makamu wa Rais ametoa wito kwa wananchi wa Mkinga kuchangamkia fursa ya uwepo wa chuo hicho ili kujipatia elimu, ujuzi na stadi za maisha zitakazowawezesha kujiajiri au kuajiriwa na kupata kipato cha kuendesha familia.

Aidha ameiagiza Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia kushughulikia changamoto ya upungufu wa vifaa vya kujifunzia katika chuo hicho ikiwemo ununuzi wa mashine kwaajili ya ukataji wa mawe ya mapambo (Tanga stone) pamoja na kuhakikisha wakufunzi wanaongezwa katika chuo hicho.

Makamu wa Rais ametoa wito kwa wakufunzi, wanafunzi na wananchi wote kutunza miundombinu ya chuo hicho ili iweze kudumu na hivyo kutoa huduma kwa vijana wengi zaidi.

Makamu wa Rais ameitaka Wizara ya Mipango na Uwekezaji kushughulikia suala la fidia halali inayopaswa kutolewa kwa wananchi waliopisha ujenzi wa kiwanda cha saruji katika Wilaya ya Mkinga.

Makamu wa Rais amesema Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan imejipanga kuona sekta ya elimu inaboreshwa ili kuchangia jitihada za kuleta maendeleo endelevu nchini. Amesema serikali itazifanyia kazi changamoto mbalimbali na kuhakikisha mazingira ya Vyuo yanaboreshwa. Aidha ametoa kutoa wito kwa wananchi, taasisi binafsi, taasisi za dini na wadau wengine wote kushirikiana na Serikali katika kutengeneza wataalamu wengi zaidi kwenye fani mbalimbali hususan za sayansi,ubunifu, teknolojia na ufundi.

Halikadhalika Makamu wa Rais amewasihi wananchi wa Wilaya hiyo kuzingatia lishe kwa watoto wakati wote ili kuwa na Taifa lenye rasilimali bora kiafya na kiakili. Pia amewasisitiza wananchi hao kutunza na kuhifadhi mazingira kwa kupanda miti na kufanya usafi.

Ujenzi wa Chuo hicho umegharimu shilingi bilioni 2.65.

Settings