Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Selemani Jafo ametoa siku Arobaini na tano (45) kwa Mwenyekiti wa Bodi ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kukamilisha Mfumo wa Kielektroniki wa Vibali vya Taka hatarishi.
Dkt. Jafo ametoa rai hiyo leo 04 Februari 2022 mara baada ya kuzindua Bodi ya Nane ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira katika Ukumbi wa St. Gaspar Jijini Dodoma
Amesema, Bodi ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira ni chombo muhimu kinachoishauri Serikali katika masuala muhimu ya Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira.
Dkt. Jafo ameitaka Bodi hiyo, kusimamia utekelezaji wa Sera ya Mazingira ya Mwaka 2021, Sheria, Kanuni na Miongozo mbalimbali ya Serikali na kuagiza kupitia upya muundo na majukumu ya Baraza ili kuimarisha utendaji wake na kutatua changamoto zilizopo katika suala zima la uhifadhi na usimamizi wa mazingira na kutoa ushauri ipasavyo.
“Mkasimamie mapato na matumizi ya fedha, simamieni Baraza kwa niaba ya Ofisi ya Makamu wa Rais ili miongozo inayotolewa na Ofisi hii iweze kutekelezwa kwa weledi” Jafo alisisitiza.
Amesema suala la mazingira ni mtambuka hivyo ni wajibu wa Bodi hiyo kuhakikisha Baraza linashirikiana na Taasisi za Serikali, Sekta binafsi na Taasisi zisizo za Kiserikali katika kusimamia hifadhi ya mazingira.
“Wengi wenu ni wabobezi katika masuala ya mazingira hivyo nina imani mtatumia taaluma na uzoefu wenu kuushauri uongozi wa Baraza katika kutekeleza majukumu yake” Alisisitiza Dkt. Jafo
Kwa upande wake Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais Bi. Mary Maganga amempongeza Mwenyekiti Prof. Esnati Chaggu na wajumbe wa Bodi hiyo kwa kuchaguliwa kuongoza Taasisi hiyo yenye jukumu kubwa la kusimamia masuala ya mazingira Nchini.
Akitoa neno la shukrani kwa niaba ya wajumbe wa Bodi, Mwenyekiti wa Bodi ya NEMC, Profesa Mhandisi Chaggu amesema Bodi ya NEMC tuna Dhamana kubwa katika kuhakikisha agenda ya mazingira inapewa msukumo wa dhati kwa kuwa ni mjadala wa dunia kwa sasa.
Tarehe 24 Januari 2022 MheshimiwaRais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan alimteua Prof. Esnati Osinde Chaggu kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa kipindi cha miaka mitatu.
Aidha, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Saidi Jafo tarehe 31 Januari 2022 aliteua wajumbe saba (7) wa Bodi ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) ambao ni Prof. Dos Santos Silayo, Prof. Hussein Hassan Sosovele, Dkt. Ezekiel Edward Mwakalukwa na Saidi Habibu Tunda. Wengine ni Dkt. Catherine Aloyce Masao, Dkt. Flora Ismail Tibazarwa na Karimu Yahya Wenge.