Makamu wa Rais aongoza Kikao cha Kamati ya Pamoja ya SJMT na SMZ, Zanzibar

Mar, 06 2024

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango ameongoza Kikao cha Kamati ya Pamoja ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SJMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) ya kushughulikia Masuala ya Muungano kilichofanyika katika Ukumbi wa Golden Tulip Zanzibar.

Makamu wa Rais amewapongeza viongozi na wataalamu wote walioshiriki katika kikao hicho kwa jitihada walizofanya wakati wa maandalizi na majadiliano. Amesema kikao hicho ni muhimu kwa mustakabali wa Taifa na Muungano hivyo ni wajibu kuhakikisha lengo la kuulinda na kuutetea Muungano linafikiwa.

Makamu wa Rais amewasihi viongozi kutambua wajibu wa Vikao vya Kamati ya Pamoja ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SJMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) vya kushughulikia Masuala ya Muungano ni kuwezesha umoja na undugu baina ya pande zote kuendelea kukua zaidi. Amesema ni vema kujadili hoja zinazoletwa kwenye vikao kwa dhati kwa kuwa wananchi wa pande zote mbili za Muungano ni wamoja.

Katika kikao hicho hoja 4 zilizosalia kati ya hoja 25 za Muungano zimejadiliwa namna ya kupatiwa ufumbuzi kutoka pande zote za Muungano. Hoja zilizojadiliwa na kuafikiwa kuendelea kutafutiwa ufumbuzi ni pamoja na Suala la Sukari, Usajili wa Vyombo vya Moto, Bodi ya Pamoja na Mgawanyo wa Mapato ya iliyokuwa Sarafu ya pamoja ya Afrika Mashariki.

Kikao hicho kimehudhuriwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla, Naibu Waziri Mkuu Mhe. Dotto Biteko, Waziri Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Selemani Jafo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili ya Rais (Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi) Mhe. Hamza Hassan Juma, Mawaziri na Manaibu Mawaziri wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Katibu Mkuu Kiongozi Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Balozi Dkt. Moses Kusiluka , Katibu Mkuu Kiongozi Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Mhandisi Zena Said, Makatibu Wakuu, Wakuu wa Taasisi pamoja na Wataalamu mbalimbali.

Settings